Jumamosi, 16 Desemba 2017

NGO’S ZINAZOKABILIANA NA UKIMWI IRINGA ZATAKIWA KUACHA ALAMA



Na. Ofisi ya mkuu wa Mkoa
Mashirika yasiyo ya kiserikali yanayopambana na maambukizi ya virusi vya Ukimwi yametakiwa kujitathmini na kuunganisha nguvu katika kupunguza maambukizi mapya ya virusi vya Ukimwi mkoani Iringa.

Kauli hiyo ilitolewa na mkuu wa Mkoa wa Iringa, Amina Masenza alipokuwa akifungua kikao cha kupitia utekelezaji wa mpango mkakati wa Mkoa wa kudhibiti maambukizi ya mapya ya virusi vya Ukimwi mkoani Iringa kikao kilifanyika katika ukumbi wa chuo kikuu Huria mjini Iringa.
 
Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Amina Masenza
Masenza alisema kuwa mashirika yasiyo ya kiserikali yote yanayoratibu masuala ya Ukimwi lazima yaache alama njema katika mkoa wa Iringa. Aliwataka kujitathmini na kuja na mkakati utakaosaidia kupunguza maambukizi mapya ya virusi vya Ukimwi.

Alisema kuwa matokeo ya utafiti wa VVU na Ukimwi umebainisha kuwa kiwango cha maambukizi kimeongezeka kwa asilimia 2.2 mkoani Iringa. Alisema kuwa ongezeko hilo ni kubwa sana. 

Lazima tupitie na kufanya tathmini ya mikakati yetu na mwanzo wa mwaka kuanza upya kwa kudumisha ushirikiano baina yetu. Yawezekana ushirikiano na dhamira ya kweli miongoni mwetu katika kupunguza maambukizi mapya haijaimarika” alisema Masenza.

Aliwataka wadau hao kuona kuwa wana deni kwa wananchi wa mkoa wa Iringa. “Kila mmoja ajisikie vibaya baada ya lile lengo tulilolitarajia hatukulifikia. Nyie wataalam lazima muweze kushauri vizuri ili tuweze kufikia dhamira ya kupunguza maambukizi mapya” alisema Masenza.

Awali afisa maendeleo ya jamii Mkoa wa Iringa, Menrad Dimoso alisema kuwa hicho ni kikao cha kazi kinacholenga kupitia utekelezaji wa mpango mkakati wa Mkoa wa kupambana maambukizi mapya ya virusi vya Ukimwi. Alisema kuwa kikao hicho kimeshirikisha wadau mbalimbali wa mapambano dhidi ya virusi vya ukimwi na halmashauri za Mkoa wa Iringa.
 
Afisa Maendeleo ya Jamii, Menrad Dimoso
Matokeo ya utafiti wa VVU na UKIMWI (2016/17) yaliyotoka hivi karibuni yalibainisha kuwa maambukizi ya VVU Mkoani Iringa yameongezeka kutoka asilimia 9.1 (2011/12) kufikia asilimia 11.3 (2016/17).
=30=

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Habari zinazoendelea hivi sasa

SERIKALI KUWEZESHA VIJANA KUKOPA

Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa Serikali itaendelea kuwawezesha vijana kwa kuwatengenezea mazingira mazuri ya mikopo ili waweze k...