Na
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Katibu Tawala Mkoa wa Iringa Bibi. Wamoja Ayubu
ameshukuru na kupongeza ushirikiano alioupata kutoka kwa watumishi wa Ofisi ya
Mkuu wa Mkoa wa Iringa na taasisi mbalimbali zilizopo mkoani hapa kipindi akiwa
Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Iringa.
Kauli hiyo ameitoka katika mapokezi ya haja
yaliyoandaliwa na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa siku yake ya kwanza ya kutumikia nafasi
yake ya Katibu Tawala Mkoa wa Iringa baada ya uteuzi na kuapishwa na Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Jakaya Kikwete.
Bibi. Ayubu ameshukuru ushirikiano huo na kusema kuwa
ushirikiano huo ndio uliomfanya kutekeleza vizuri majukumu yake akiwa Kaimu
Katibu Tawala wa Mkoa wa Iringa. Aidha, ametoa wito kwa watumishi wote na
taasisi mbalimbali kuendelea kumpatia ushirikiano ili kufanikisha utekelezaji
wa majukumu ya mkoa wa Iringa na Taifa kwa ujumla.
Akiongelea matarajio yake kwa wananchi wa mkoa wa
Iringa, amesema kuwa hana wasiwasi na wananchi wa mkoa wa Iringa kutokana na
uchapa kazi wao na kujituma katika kutekeleza majukumu ya serikali. Aisha,
amewaomba wananchi kuendelea kutoa ushirikiano kwake ili pamoja kuuletea
maendeleo mkoa wa Iringa.
Bibi. Wamoja ametumia fursa hiyo kushukuru
ushirikiano aliopatiwa katika maadhimisho ya kilele cha mbio za Mwenge wa Uhuru
kitaifa kilichofanyika mkoani Iringa.
Katibu Tawala Mkoa wa Iringa amemshukuru Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kumteua katika nafasi hiyo na kuahidi kuwa
atatekeleza majukumu yake kwa juhudi na maarifa.
Kwa upande wake Katibu Tawala Msaidizi, Sehemu ya Uchumi
na Sekta za Uzalishaji, Adam Swai ameutaja uteuzi uliofanywa na Rais Dkt.
Kikwete kuwa ni faraja kubwa kwa watumishi na wananchi wa mkoa wa Iringa.
Amemtaja Bibi. Ayubu kuwa ni mchapa kazi mzuri anayetoa ushauri mzuri kwa
watumishi walio chini yake.
Aidha, amewataka watumishi na viongozi wote
kumpatia ushirikiano unaostahili hasa katika kindi hiki ambapo mkoa wa Iringa
unahitaji kuzalisha chakula kwa wingi.
Ikumbukwe kuwa Bibi. Wamoja Ayubu anakuwa Katibu Tawala
wa Mkoa wa Iringa akipokea kijiti kutoka kwa Katibu Tawala Mstaafu Bibi.
Gertrude Mpaka aliyestaafu mwaka 2012.
=30=
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni