Jumamosi, 26 Aprili 2014

MIAKA 50 YA MUUNGANO IMELETA MAFANIKIO NCHINI



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Mkuu wa Mkoa wa Iringa amesema kuwa Muungano wa Tanganyika na Zanzibar umeleta mafanikio makubwa katika nyanja zote nchini.
Mwakilishi wa Mkuu wa Mkoa wa Iringa ambaye ni Kaimu Katibu Tawala Mkoa, Bibi. Scolastica Mlawi (katikati) akifuatilia burudani mbalimbali

Kauli hiyo imetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma katika hotuba yake iliyosomwa kwa niaba yake na Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Iringa Scolastica Mlawi katika Maadhimisho ya miaka 50 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar yaliyofanyika katika kijiji cha Kasanga, Kata ya Kasanga, Tarafa ya kasanga wilayani Mufindi.

Dkt. Ishengoma amesema “muungano umeleta manufaa makubwa katika nyanja za kisiasa, kiuchumi, kijamii na kiutamaduni, jukumu letu ni kuuenzi, kuudumisha na kuuimarisha kwa masilahi ya vizazi vya sasa na vijavyo”.  Amesema kuwa manufaa yatokanayo na Muungano huu ni pamoja na kudumishwa kwa amani, upendo, umoja, mshikamano na ushirikiano miongoni mwa jamii ya Tanzania Bara na Tanzania visiwani.

Mkuu wa Mkoa wa Iringa amesema kuwa waasisi wa Muungano walikubaliana kushirikiana katika mambo mengi. Ameyataja baadhi ya mambo hayo kuwa ni katiba na serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mambo ya nchi za nje, ulinzi na usalama, polisi, mamlaka juu ya mambo yanayohusika na hatari. Mambo mengine ni pamoja na uraia, uhamiaji, mikopo na biashara za nje, utumishi katika serikali ya Jamhuri ya Muungano na kodi inayolipwa na watu binafsi na mashirika. Ameyataja mambo mengine kuwa ni ushuri wa forodha na ushuru wa bidhaa zinazotengenezwa nchini unaosimamiwa na idara ya forodha pamoja na ushirikiano wa bandari, usafiri wa anga na posta na simu.

Dkt. Ishengoma amewataka wananchi wote mkoani Iringa kuhakikisha wanaendeleza yale yote mambo mazuri yaliyoachwa na waasisi wa Muungano na kuyaboresha pale inapobidi. Aidha, amewataka wananchi wote kujitokeza na kushiriki katika shughuli za maendeleo ili kujiletea maendeleo ya kijamii na kiuchumi.    

Maadhimisho ya miaka 50 ya Muungano wa Tanzania yameongozwa na kauli mbiu isemayo “Utanzania Wetu ni Muungano Wetu, Tuulinde, Tuuimarishe na Kuudumisha”.
=30=

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Habari zinazoendelea hivi sasa

SERIKALI KUWEZESHA VIJANA KUKOPA

Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa Serikali itaendelea kuwawezesha vijana kwa kuwatengenezea mazingira mazuri ya mikopo ili waweze k...