Jumamosi, 26 Aprili 2014

WIKI YA CHANJO MKOANI IRINGA

Na. Dajari Mgidange
Wazazi wametakiwa kuwapeleka watoto wao wenye umri chini ya miaka miwili kwenye vituo vya huduma za afya kupatiwa chanjo dhidi ya magonjwa mbalimbali.

Kaul;I hiyo imetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma alipokuwa akizindua wiki ya chanjo katika mkoa wa Iringa uzinduzi uliofanyika katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa.

Dkt. Christine amesema kuwa kumekuwa na ongezeko la watoto ambao hawajapata na wengine kutokamilisha chanjo zao matokeo yake kusababisha milipuko ya magonjwa ya mara kwa mara hasa ugonjwa wa surua. Amesema katika jitihada za kuzuia milipuko hiyo Tanzania inatarajia kutoa chanjo ya pili ya surua mwaka huu. Ametoa wito “kwa wazazi na walezi kuwapeleka watoto wote wenye umri chini ya miaka miwili ambao hawajapata chanjo au hawajakamilisha chanjo zao kwenye vituo vya huduma za afya wakiwa na kadi zao za kliniki lakini pia watoto ambao hawana kadi wapelekwe watapewa kadi na chanjo” alisisitiza Dkt. Ishengoma.

Amesema “kila mmoja wetu anawajibu wa kuhakikisha kuwa mtoto wake, mtoto wa jirani au mlengwa mwingine yeyote anapewa chanjo ili kuzuia asipatwe na maradhi ambayo yanakingwa na chanjo na asiwe hatari kwa wengine kwa kuwaletea ugonjwa”. Amesema kuwa chanjo ni jukumu la jamii nzima na hutolewa bila malipo yoyote na kuwahakikishia kuwa hazina madhara yoyote.

Mkuu wa Mkoa amesema kuwa wiki ya chanjo ni fursa ya kutoa ujumbe kuhusu chanjo mpya za kuzuia ugonjwa wa Nimonia na Kuhara kwa watoto na kuhamasisha jamii kufika vituoni ili kupata maelezo zaidi na huduma hiyo. Ujumbe wa wiki ya chanjo ni “Jamii iliyokamilisha chanjo ni jamii yenye Afya” ukiongozwa na kaulimbiu isemayo “Chanjo ni jukumu  letu sote”.

Amesema kuwa chanjo ni mkakati muafaka katika kutokomeza maradhi na kupunguza vifo vya watoto, hivyo kupunguza gharama kubwa kwa famila na Taifa kwa ujumla. Ameongeza kuwa chanjo huchangia kupunguza vifo vya watoto kati ya milioni mbili (2) hadi milioni tatu (3) Duniani kila mwaka yakiwemo maradhi ya Nimonia na Kuhara ambayo yamekua ni chanzo cha vifo vingi. Ameyataja magonjwa yanayokingwa hapa nchini na chanjo kuwa ni kifua kikuu, dondakoo, polio, surua, pepopunda, homa ya ini, homa ya uti wa mgongo, kichomi na kuhara.

Tanzania inaungana na nchi nyingine katika kuadhimisha wiki ya chanjo Duniani tarehe 24-30 April 2014. Katika mkoa wa Iringa ilizinduliwa katika kijiji cha Ulata Kata ya Wasa, Tarafa ya Kiponzelo katika Halmashauri ya Wilaya ya Iringa.
=30=

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Habari zinazoendelea hivi sasa

SERIKALI KUWEZESHA VIJANA KUKOPA

Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa Serikali itaendelea kuwawezesha vijana kwa kuwatengenezea mazingira mazuri ya mikopo ili waweze k...