Ijumaa, 2 Mei 2014

KALALU AWAPONGEZA WAFANYAKAZI MUFINDI



Na. Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Mufindi
Mkuu wa wilaya ya Mufindi Evarista Kalalu amewapongeza wafanyakazi wilayani Mufindi kwa kazi nzuri wanayofanya katika kukuza uchumiwa wilaya hiyo.

Kauli hiyo imetolewa katika hotuba yake iliyosomwa kwa niaba yake na Katibu Tawala Wilaya ya Mufindi Allan Benard katika maadhimisho ya siku ya wafanyakazi duniani iliyofanyika mjini Mafinga.

Kalalu amesema kuwa anawapongeza wafanyakazi wote kwa kazi nzuri wanayofanya na kuinua uchumi wa wilaya ya Mufindi. Akiongelea wafanyakazi bora amesema “nawapongeza wafanyakazi wote watakaopewa tuzo ya kuwa wafanyakazi bora katika sehemu zao za kazi. Hongereni sana kwa mafanikio haya. Nina uhakika kwamba wapo wafanyakazi wengine wengi ambao wanafanya kazi kwa bidii katika maeneo yao ya kazi lakini hawakubahatika kupata tuzo. Naomba wasikate tamaa, waendelee kuchapa kazi.  Huenda na wao watabahatika Mei Mosi ijayo”. 

Aidha, amewataka wafanyakazi kufanya kazi kwa bidii, umahiri na weledi ili kuongeza tija kwenye maeneo yao. Amesema “mnayo nafasi kubwa ya kuchangia maendeleo ya nchi yetu na watu wake. Nawaomba muitumie vizuri nafasi hiyo” alisisitiza Kalalu.

Akiongelea ujumbe wa kaulimbiu, Mkuu wa Wilaya ya Mufindi amesema kuwa kauli mbiu isemayo utawala bora utumike kutatua kero za wafanyakazi” ni kauli mbiu yenye ujumbe mzuri ambao unasisitiza masuala yote ya maamuzi ya kiutendaji na kiutekelezaji katika shughuli za kila siku za Serikali yazingatie sheria, kanuni na taratibu za kiserikali zilizowekwa. 

Amesema kuwa mwajiri anapaswa kutoa ushirikiano mkubwa kwa watumishi wake ikiwa ni pamoja na wajibu wa kutoa vitendea kazi bora, kujali usalama na masilahi ya wafanyakazi yakiwemo masuala ya afya, mishahara inayoendana na hali halisi ya maisha kwa wakati husika. Amesema kuwa mfanyakazi anapaswa kuelewa umuhimu wa nafasi yake katika jamii kwa kufanya kazi kwa juhudi, maarifa na nidhamu ili kuleta tija. 

Akijibu risala ya wafanyakazi, Mkuu wa Wilaya ya Mufindi amesema kuwa Serikali imepokea mapendekezo ya kuangalia upya suala la kodi inayotozwa kwenye mishahara ya wafanyakazi na kupanda kwa kima cha chini cha mshahara kufikia Tshs. 315,000/= kwa mwezi. Masuala mengine ambayo serikali inaendelea kuyafanyia kazi ni uwiano kwa maslahi ya mifuko ya jamii na wastaafu kupewa mafao yao kwa muda muafaka. “Napenda kuwahakikishia kuwa Serikali imepokea ushauri na mapendekezo hayo na itayafanyia kazi na tutapeana taarifa ya maendeleo ya utekelezaje wake alisisitiza Mkuu wa Wilaya. 

Kalalu amesema kuwa Serikali inaendelea na mikakati ya kuimarisha utendaji kazi na uwajibikaji Serikalini ili wananchi wahudumiwe vizuri  kama inavyostahili. Amesema kuwa serikali imeanzisha mfumo mpya wa ufuatiliaji na tathmini ya utekelezaji wa maeneo ya kipaumbele ya Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano kwa lengo ni kuboresha na kuharakisha utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025.  Mfumo huo unatokana na mifano mizuri inayotumika katika nchi kadhaa duniani ambako umewaletea ufanisi mkubwa.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Habari zinazoendelea hivi sasa

SERIKALI KUWEZESHA VIJANA KUKOPA

Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa Serikali itaendelea kuwawezesha vijana kwa kuwatengenezea mazingira mazuri ya mikopo ili waweze k...