Ijumaa, 2 Mei 2014

WAFANYAKAZI IRINGA WATIMIZE WAJIBU

NA FRANK KIBIKI, IRINGA
MKUU wa mkoa wa Iringa, Dk Christine Ishengoma amewataka wafanyakazi wasiotimiza wajibu wao kuacha tabia hiyo, ili  kutokwamisha jitihada za wananchi kujipatia maendeleo.
 
Akizungumza Katika hotuba yake, iliyosomwa na Mkuu wa Wilaya ya Iringa Dk Letisia Warioba, katika maadhimisho ya Mei mosi yambayo kwa mkoa huo, yalifanyika katika kijiji cha Isimani, Dk Ishengoma alisema inasikitisha kuona kuwa wapo baadhi ya wafanyakazi ambao badala ya kufanya kazi kwa bidii, wamekuwa wakisababisha huduma za jamii kuzorota.
 
Alisema wapo baadhi ya wafanyakazi ambao kwa maksudi wamekuwa wakiendekeza vitendo vya rushwa na kuwafanya wananchi kukosa huduma wanazostahili kwa mujibu wa taratibu.
 
“Rushwa imekuwa ikisababisha mwenye haki kudhulumiwa haki yake na kupatiwa mtu asiyestahili kupata haki hiyo, ndugu zangu wafanyakazi siku hii tusiitumie kudai haki zetu za kulipwa vizuri na kuandaliwa masingira mazuri ya kazi tu, bali tujiulize je tumetimiza wajibu wetu?” alisema Dk Ishengima.
 
Alisema mbali na rushwa baadhi ya wafanyakazi wamekuwa wakichelewa kufika katika maeneo yao ya kufanyia kazi jambo ambalo, linaendelea kudumaza utoaji wa huduma.
 
Mbali na uchelewaji, Dk Ishengoma alisema kuwa wapo ambao wamekuwa wakiwahi kufika kazini, lakini hawawajibiki ipasavyo na kusababisha huduma kudorora.
 
Aliitaja kasoro nyingine kuwa ni ubadhilifu wa mali za ofisi jambo linalosababisha walengwa waliokusudiwa kukosa huduma iliyokuwa imepangwa kutolewa kwao.
 
Alipiga marufuku, mavazi yasiyo na staha kwa Wafanyakazi jambo linalosababisha kudharauliwa kwa Mfanyakazi sambamba na kukemea tabia ya kuvujisha siri za ofisi kwa madai kuwa hilo pia ni tatizo linalohitaji kuangaliwa kwa jicho la pekee.
 
Aliwapongeza wafanyakazi ambao, kwa kipindi cha mwaka mzima wamekuwa wakitimiza wajibu wao na kuwataka wale ambao kwa njia moja au nyingine wamekuwa wakizorotesha maendeleo, kuacha.
 
Alisema hatua kali z akisheria zitaendelea kuchukuliwa kwa wafanyakazi wasiotimiza wajibu wao, ili kwa pampoja wasaidiane kuongeza kasi ya ukuaji wa maendeleo na huduma za jamii mkoani humo.
 
Alivitaka vyama vya wafanyakazi, kusaidia katika kutoa elimu kwa wanachama wao ili kila mmoja atimize wajibu wake akiwa kazini.
 
“Tutimize kwanza wajibu wetu ndipo tudai maslahi yetu, kama kila mmoja atafanya kazi kwa bidii ni rahisi kufikia malengo ya kudai mashali yetu, uvivu, tamaa na wizi ni adui wa maendeleo yetu,” alisema Dk Ishengoma.
 
Alisema serikali itaendelea kutekeleza ahadi zake, za kutatua kero zinazowakabili wafanyakazi wa sekta zote ili kila mmoja apate stahili yake.
 
Awali katika risala yao, wafanyakazi hao waliiomba serikali kuendelea kutatua kero zinazowakabili na kukwamisha jitihada yao katika kufanya kazi.
 
Walizitaja kero hizo kuwa ni pamoja na mishahara midogo, mazingira magumu ya kazi kwa baadhi ya sekta, makato makubwa ya kodi, malipo ya madeni yao ikiwemo hamisho na malimbikizo ya mishahara.
 
Mwisho
@MUITIKIO

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Habari zinazoendelea hivi sasa

SERIKALI KUWEZESHA VIJANA KUKOPA

Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa Serikali itaendelea kuwawezesha vijana kwa kuwatengenezea mazingira mazuri ya mikopo ili waweze k...