Jumatano, 25 Juni 2014

WANAOVURUGA MCHAKATO WA KATIBA MPYA WAPUUZWE



Na. Frank Kibiki- KILOLO
WATANZANIA wametakiwa kuwapuuzia na kutowafuata wanasiasa wachache wenye uchu wa madaraka na  nia ya kuvuruga mchakato wa kupata katiba mpya, unaeondelea hapa nchini.
Kiongozi wa mbio za Mwenge, Rahel Kassanda alitoa wito huo wilayani Kilolo, mkoani Iringa wakati akizungumza na wakazi wa wilaya hiyo juu ya ujumbe wa mwenge wa uhuru kwa mwaka huu, unaohamasiaha wananchi kushiriki katika mchakato huo.
Kassanda alisema wapo baadhi ya wanasiasa wachache ambao wameonekana wazi wakitaka kuvuruga mchakato wa katiba mpya, ambao Rais Jakaya Kikwete aliuasisi ili kuhakikisha katiba hiyo ambayo kwa mara ya kwanza imeshirikisha wananchi, inapatikana.
“Wapuuzeni hawa wanasiasa wachache ambao wanaonekana wakitaka kuvuruga mchakato wa katiba mpya kwa maslahi yao wenyewe, achaneni nao nanyi mjitokeze kupiga kura mara zoezi hili litakapokuwa tayari, Tanzania sasa tunahitaji katiba mpya,”alisema.
Awali mkuu wa mkoa wa Iringa, Dk Christine Ishengoma alitoa wito kwa wananchi wa mkoa huo kujiandaa na zoezi la kupiga kura ya maoni ya rasimu ya katiba mpya wakati muda utakapofika, ili watumie ipasavyo haki yao ya msingi kikatiba.
Akipokea Mwenge wa uhuru aliokabidhiwa na Mkuu wa mkoa wa Morogoro, Joel Bendera Dk Ishengoma alisema ni wajibu wa kila mkazi wa mkoa huo kutumia haki hiyo kikatiba.
“Ujumbe huu ni muhimu sana hasa katika kipindi hiki ambacho watanzania tunapaswa kushikamana zaidi na kuwa wamoja tunapoelekea katika kukamilisha mchakato wa kupata katiba mpya, ambayo itakuwa dira ya kuliongoza taifa hili sasa na miaka ijayo,”alisema Dk Ishengoma.
Alisema katika kuhakikisha wananchi wa mkoa huo wanashiriki kikamilifu kwenye mchakato wa katiba mpya, serikali inashirikisha wadau wengine kuendelea kutoa elimu kwa jamii ili ione suala hilo linawahusu moja kwa moja.
Dk Ishengoma aliwataka wananchi wa mkoa huo kuendelea kudumisha amani, utulivu na mshikamano ikiwa ni pamoja na kuepukana na tabia ambazo zinaweza kuhatarisha mambo hayo.
“Wananchi wa Iringa wanaimani kubwa kwamba sasa watapata katiba mpya, ambayo italiongoza taifa kwa miaka mingi ijayo, huku dira ikiwa kuendelea kuwa na taifa imara,”alisema mkuu huyo wa Mkoa.
Alisema Mwenge huo ukiwa mkoani Iringa, utazindua miradi 42 yenye thamani ya zaidi ya sh bilioni 3.1.
Aliitaja miradi hiyo kuwa ni ya sekta za kilimo, barabara, elimu, afya, maji na maendeleo ya jamii vikiwemo vikundi vya kiuchumi.
Mwisho.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Habari zinazoendelea hivi sasa

SERIKALI KUWEZESHA VIJANA KUKOPA

Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa Serikali itaendelea kuwawezesha vijana kwa kuwatengenezea mazingira mazuri ya mikopo ili waweze k...