Ijumaa, 1 Agosti 2014

WAKUU WA MIKOA IRINGA, NJOMBE NA MBEYA WADUMISHE AMANI



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa - IRINGA
Wakuu wa Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini watakiwa kudumisha amani na usalama ili kuvutia uwekezaji endelevu kwa lengo la kukuza uchumi na kipato cha mtu mmojammoja.

Kauli hiyo imetolewa na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mizengo Pinda alipokuwa akifungua Kongamano la uwekezaji Nyanda za Juu Kusini lililofanyika leo jijini Mbeya.

Pinda amesema kuwa hakuna uwekezaji endelevu na wenye tija katika maeneo yenye fujo, vurugu na uvunjifu wa amani. Amesema kuwa uwekezaji wenye tija mara zote hufanyika katika maeneo yenye utulivu mkubwa na amani. Aidha, ameutaka uongozi wa mikoa hiyo kutoa nafasi kubwa ya ushirikiano baina ya sekta binafsi na sekta ya umma kutokana na umuhimu wao katika kuleta maendeleo.  

Akiongelea umuhimu wa kongamano hilo, Waziri Mkuu  amesema kuwa lengo la kongamano hilo ni kuibua fikra mpya za mikoa na kanda kujiamini kuwa wanauwezo wa kuvuta fursa za uwekezaji na kukuza uchumi, kuongeza pato la taifa na kupambana na umasikini kwa wananchi. Amesema kuwa wawekezaji wameanza kuona Dar es Salaam si mahali pekee pa kuwekeza tatizo wanalokumbana nalo hawajapata taarifa za maeneo yenye fursa za uwekezaji.

Waziri Mkuu ameitaka kanda hiyo kujipanga vizuri katika kilimo cha mbogamboga na matunda kwa lengo la kuinua pato la mikoa hiyo.

Akiongelea kilimo cha mahindi, Waziri Pinda amesema kuwa nchi ya Tanzania ni ya tano katika Afrika kwa uzalishaji wa mahindi ikishika nafasi ya 15 duniani. Ameitaja changamoto kuwa Tanzania ni nchi ya mwisho katika makundi yote mawili katika tija na kuitaka mikoa hiyo kuongeza tija katika kilimo cha mahindi na usindikaji wake. Aidha, ameitaka mikoa hiyo kujipanga kimvuto wa viwanda vya mbolea ili kuhakikisha mbolea inakuwepo ya kutosha na kwa gharama za kawaida.

Akiongelea sekta ya mifugo katika ukanda huu, Waziri Mkuu amesema kuwa wakati kanda hiyo ikijivunia wingi wa mifugo ikiwa na  ng’ombe zaidi ya 1,000,000 na mbuzi zaidi ya 500,000 inakabiliwa na changamoto ya viwanda vya usindikaji nyama. Aidha, amemuagiza Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu- Dkt. Mary Nagu kuhakikisha kiwanda cha kusindika nyama cha Mbeya kinaanza kazi mara moja kwa kuwataka wadau wote kukaa pamoja na kutoka na suluhisho.

Waziri Mkuu amewahakikishia wawekezaji umeme wa uhakika. Amesema kuwa serikali imejipanga kuwa na umeme wa kutosha nchini ifikapo mwaka 2015. Amezitaka mamlaka za serikali za mitaa kuondoa umangimeza na vikwazo visivyo vya lazima katika kuhamasisha uwekezaji. “Msiwe kikwazo, kuweni wawezeshaji. Ninyi si watawala ni waleta maendeleo katika jamii” alisisitiza Waziri Mkuu.

Kongamano la uwekezaji kwa mikoa ya Iringa, Njombe na Mbeya ni muitikio wa agizo la Waziri Mkuu, Mizengo Panda kuhakikisha makongamano yanafanyika katika ngazi ya kanda ili kuweza kuvutia wawekezaji nchini kwa lengo la kukuza uchumi nchini.
MWISHO

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Habari zinazoendelea hivi sasa

SERIKALI KUWEZESHA VIJANA KUKOPA

Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa Serikali itaendelea kuwawezesha vijana kwa kuwatengenezea mazingira mazuri ya mikopo ili waweze k...