Alhamisi, 8 Januari 2015

WANANCHI WATAKIWA KUSHIRIKI KATKA UTUNZAJI WA BARABARA IRINGA



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Ushiriki hasi wa jamii juu ya utunzaji wa barabara ni kichocheo kikubwa cha uharibifu wa barabara mkoani Iringa.

Kauli hiyo imetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Amina Masenza alipokuwa akifungua kikao cha bodi ya barabara Mkoa wa Iringa kilichofanyika katika ukumbi wa Siasa ni Kilimo mjini Iringa.

Masenza amesema “katika kuhakikisha tunakuwa na barabara zinazopitika muda wote, nimeona mapungufu ya ushiriki wa jamii juu utunzaji wa barabara hizo. Wananchi wamekuwa wakifanya shughuli ndani ya hifadhi ya barabara na kuacha uchafu kwenye barabara na uchafu huo kuziba mifereji na kuharibu barabara hizo hasa kipindi hiki cha mvua.” Amezitaka mamlaka husika kuendelea kutoa elimu kwa wananchi ili washiriki kikamilifu katika utunzaji wa barabara hizo kutokana na kuwa na manufaa kwa wananchi wote. Amesema kuwa barabara hizo zimeendelea kuwa muhimu hasa kwa wakulima kuwezesha kusafirisha mazao yao haraka na unafuu kuyapeleka sokoni.

Akiongelea kipindi hiki cha mvua, Mkuu wa Mkoa amesema kuwa kipindi hiki jamii inakabiliwa na changamoto lukuki yakiwemo maafa yanayosababishwa na mvua. Amezitaka mamlaka husika kufuatilia na kurekebisha maeneo korofi ili barabara katika maeneo hayo ziweze kupitika muda wote. Ameyataja maeneo yanayotakiwa kuangaliwa kwa umakini zaidi kuwa ni matengenezo ya mifereji, makaravati na madaraja. 

Aidha, amewataka Wakala wa barabara Mkoa wa Iringa na Halmashauri kuwasimamia vizuru wakandarasi ili wafanye kazi kwa umakini na uhakika mkubwa ili barabara ziweze kudumu. Vilevile, ametaka elimu iendelee kutolewa kwa wananchi kutokujenga katika maeneo yenye uwezekano wa kupata mafuriko. 
=30=

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Habari zinazoendelea hivi sasa

SERIKALI KUWEZESHA VIJANA KUKOPA

Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa Serikali itaendelea kuwawezesha vijana kwa kuwatengenezea mazingira mazuri ya mikopo ili waweze k...