Jumapili, 1 Machi 2015

PINDA APONGEZA KILIMO KATIKA SKIMU YA NYANZWA



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Wananchi wa vijiji vya Nyanzwa na Igunda wamepongezwa kwa juhudi kubwa za kuendeleza kilimo katika eneo linalozunguka skimu ya umwagiliaji ya Nyanzwa.
Pongezi hizo zimetolewa na Waziri Mkuu Mhe. Mizengo Pinda baada ya kukagua skimu hiyo iliyopo katika Wilaya ya Iringa.
Mhe. Pinda amesema “nawapongeza wakulima na wananchi wa Nyanzwa na Igunda kwa juhudi kubwa za kuendeleza kilimo katika eneo hilo. Nitoe wito kwa uongozi wa kata na vijiji vya Nyanzwa na Igunda kuendelea kutunza chanzo cha maji ya umwagiliaji katika skimu ya Nyanzwa”. Amewataka kushirikiana na uongozi wa Halmashauri kuweka mipaka ya chanzo cha maji na kuweka utaratibu endelevu wa kukitunza.
Amesema historia inaonesha kuwa chanzo cha maji cha Nyanzwa kilikuwa na uwezo mkubwa wa kumwagilia hekta 940 na kuutaka uongozi wa Mkoa na Halmashauri ya Wilaya ya Kilolo kukaa na kuandaa mpango mahususi wa kuendeleza skimu ya umwagiliaji na kufanya mapitio ya upembuzi yakinifu iliyofanyika awali ili kuweza kuingiza mradi huo katika mpango na bajeti ya Halmashauri ya Kilolo kwa mwaka 2015/2016.
Katika kutoa msukumu kwa wakulima kupata mitaji ya kilimo, Mhe. Pinda alishauri Halmashauri ya Wilaya ya Kilolo isaidie vijiji vya Nyanzwa na Igunda kufufua jumuiya yao ya ushirika iliyokuwa inaundwa na vijiji vya Nyanzwa, Igunda na Mgowelo au kuunda SACCOS mpya ambayo ni imara zaidi na kuwataka Maafisa Ushirika wawasaidie wakulima kuunda chombo hicho.
Kutokana na hali ya kijiografia na fursa kubwa ya kuendeleza ufugaji nyuki katika vijiji vya Nyanzwa na Igunda, Waziri Mkuu aliushauri uongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilolo kutazama uwezekano wa kuanzisha mradi wa ufugaji nyuki kwa lengo la kuongeza kipato cha wananchi. 
=30=

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Habari zinazoendelea hivi sasa

SERIKALI KUWEZESHA VIJANA KUKOPA

Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa Serikali itaendelea kuwawezesha vijana kwa kuwatengenezea mazingira mazuri ya mikopo ili waweze k...