Jumapili, 23 Julai 2017

IRINGA YAANDAA MAZINGIRA WEZESHI KWA VIJANA



Na. Dennis Gondwe, Iringa
Serikali imeandaa mazingira wezeshi kwa ajili ya vijana kujiajiri katika mkakati wake wa kukabiliana na tatizo la ajira nchini.

Kauli hiyo ilitolewa na mkuu wa mkoa wa Iringa, Amina Masenza alipokuwa akiongea na kaimu Balozi wa Marekani nchini, Inmi Patterson aliyefanya ziara ya kikazi mkoani Iringa na kumtembelea ofisini kwake jana.
Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Amina Masenza

Masenza alisema kuwa serikali imeandaa mazingira mazuri na wezeshi kwa ajili ya vijana kujiajiri nchini na mkoa wa Iringa unaendelea kusimamia utekelezaji huo. Alisema kuwa mazingira hayo ni mkakati wa kuwafanya vijana wafikirie kujiajiri zaidi kuliko kuajiriwa na serikali kwa sababu serikali haiwezi kuwaajiri vijana wote nchini. 

Muitikio wa vijana kujiajiri ni mkubwa, mfano katika sekta ya kilimo vijana wengi wamejiajiri na kupata matokeo mazuri katika mavuno hivyo kukuza kipato chao na wengine kuajiri wenzao kupitia kilimo” alisema Masenza.

Kaimu Balozi wa Marekani nchini Tanzania, Inmi Patterson alipongeza juhudi hizo za serikali na uongozi wa mkoa wa Iringa katika kutengeneza mazingira mazuri ya ajira kwa vijana. “Kwa mipango hiyo, kuna mustakabali mzuri kwa vijana” alisema Patterson. 

Aidha, alisisitiza kuwa elimu kwa vijana ni muhimu katika kufikia maendeleo ya kiuchumi na kijamii. “Vijana bila elimu hakuna maendeleo” alisema Patterson.

Akiongelea utawala bora katika sekta ya afya, Katibu Tawala Mkoa wa Iringa, Wamoja Ayubu alisema kuwa mkoa wa Iringa umepiga hatua katika dhana ya utawala bora na uwazi katika sekta ya afya. “Mkoa wa Iringa umeendelea kuimarisha uwazi katika utoaji huduma ili kuondoa mianya ya rushwa. Huduma zinazotolewa katika hospitali zetu pamoja na gharama zake zimebandikwa katika mbao za matangazo ili wananchi waweze kufahamu” alisisitiza Ayubu.

=30= 








Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Habari zinazoendelea hivi sasa

SERIKALI KUWEZESHA VIJANA KUKOPA

Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa Serikali itaendelea kuwawezesha vijana kwa kuwatengenezea mazingira mazuri ya mikopo ili waweze k...