Jumapili, 23 Julai 2017

MAREKANI YAPONGEZA UTENDAJI KAZI WA JPM



Na. Dennis Gondwe, Iringa
Marekani yapongeza jitihada zinazofanywa na Rais Dk John Magufuli za kupambana na ufisadi nchini.

Pongezi hizo zilitolewa na kaimu Balozi wa Marekani nchini, Inmi Patterson alipomtembelea Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Amina Masenza ofisini kwake hivi karibuni akiwa katika ziara ya kikazi. Patterson alisema kuwa ubalozi wake unatambua juhudi zinazofanywa na Rais Dk Magufuli za kupambana na ufisadi nchini. Aidha, alisema kuwa amefurahishwa na kauli ya Rais Dk Magufuri ya rushwa haivumiliki kwa namna yoyote. Aliongelea juhudi zinazofanywa katika maeneo ya kukuza demokrasia, afya, elimu, uchumi na maendeleo kuwa ni maeneo ya kipaombele.

Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Amina Masenza alisema kuwa mkoa wake unaendelea na mapambano dhidi ya rushwa kwa kuwahimiza wananchi kufichua vitendo vyote vya rushwa na viashiria vyake na pindi watuhumiwa wanapobainika hatua za kisheria zinachukuliwa mara moja. 

Aliongeza kuwa masanduku ya maoni yamewekwa katika maeneo mbalimbali ili kuwawezesha wananchi kutoa maoni yao juu ya utendaji kazi na malalamiko dhidi ya vitendo vya rushwa katika kuimarisha utawala bora. 

Vilevile, aliongelea mkakati wa kupandikiza dhana ya kuikataa rushwa kwa vijana wakiwa shuleni, Mkuu wa Mkoa alisema kuwa klabu za kupinga rushwa zimeanzishwa katika shule za sekondari za mkoa wa Iringa.

Akiongelea utawala bora katika sekta ya afya, Katibu Tawala Mkoa wa Iringa, Wamoja Ayubu alisema kuwa mkoa wa Iringa umepiga hatua katika dhana ya utawala bora na uwazi katika sekta ya afya. 

Mkoa wa Iringa umeendelea kuimarisha uwazi katika utoaji huduma ili kuondoa mianya ya rushwa. Huduma zinazotolewa katika hospitali zetu pamoja na gharama zake zimebandikwa katika mbao za matangazo ili wananchi waweze kufahamu” alisisitiza Ayubu.

=30= 









Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Habari zinazoendelea hivi sasa

SERIKALI KUWEZESHA VIJANA KUKOPA

Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa Serikali itaendelea kuwawezesha vijana kwa kuwatengenezea mazingira mazuri ya mikopo ili waweze k...