Ijumaa, 8 Septemba 2017

CHANGAMOTO ZAFUNIKA MAFANIKIO USTAWI WA JAMII IRINGA

Na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Changamoto zinazovikabili vitengo vya ustawi wa jamii katika Halmashauri mkoani Iringa zimekuwa vikifunika mafanikio yanayopatikana kutokana na utendaji wa maafisa ustawi wa jamii.

Kauli hiyo ilitolewa na afisa ustawi wa jamii wa Halmashauri ya wilaya ya Mufindi, Elisha Nyamara alipokuwa akiwasilisha taarifa ya utendaji kazi wa shughuli za ustawi wa jamii ngazi ya Halmashauri katika kikao cha uhamasishaji wa shughuli za ustawi wa jamii kwa kamati ya ulinzi na usalama mkoa wa Iringa na wataalam wa ofisi ya mkuu wa mkoa jana.

Nyamara alisema “kitengo cha ustawi wa jamii kimekuwa na kinakabiliwa na changamoto kadhaa ambazo zinafanya wakati mwingine kuonekana kuwa majukumu ya maafisa ustawi wa jamii hayatekelezeki ipasavyo lakini ukweli ni kuwa changamoto huziba mafanikio na kufanya mapungufu katika utendaji kuonekana zaidi”. 

Aliongeza kuwa changamoto hizo zinasababishwa na mifumo, uelewa, ufinyu wa bajeti na uwezo mdogo wa maafisa ustawi kwa baadhi ya Halmashauri.

Nyamara alizitaja changamoto hizo kuwa ni uchache wa watumishi. “Uchache wa watumishi ni changamoto kubwa, kwasasa kwenye Halmashauri zote tano, kuna watumishi 14 tu badala ya watumishi 40 kwenye ngazi ya Halmashauri huku kukiwa hakuna mtumishi yeyote wa ustawi wa jamii kwenye ngazi ya kata. 

Ni maafisa hao hao wanaopaswa kwenda mahakama ya watoto na ile ya wilaya, kwenda katani na vijijini kufanya uchunguzi wa kijamii dhidi y ukatili, kwenda dawati la jinsia na watoto na pia kupokea na kusikiliza migogoro ya ndoa na yote haya ni matakwa ya kisheria” alisema Nyamara.

Changamoto nyingine aliitaja kuwa ni kitengo kupewa kiasi kidogo cha fedha katika bajeti ya mapato ya ndani na kusababisha kushindwa kutekeleza shughuli husika.

Wakati mwingine hata bajeti unayopewa inaonekana kwenye kitabu lakini wakati wa kuiomba kutekeleza shughuli husika unaambiwa hakuna fedha. Jambo hili linachangiwa na mambo mengi ikiwemo watoa maamuzi kukosa uelewa juu ya ustawi wa jamii, au kwa vile kisiasa mambo haya hayawajengi zaidi wahusika au wakati mwingine kukosa mtu wa kusemea shughuli hizi katika vikao vya maamuzi au utendaji” alisema Nyamara.

Changamoto nyingine ilitajwa na afisa ustawi wa jamii kuwa ni ufinyu wa majengo ya ofisi za ustawi wa jamii kwenye Halmashauri. “Ofisi za kitengo cha ustawi wa jamii hufikiriwa katika mtazamo wa watumishi husika kukaa na kufanya kazi lakini kwamba panahitajika faragha katika utendaji kazi jambo hilo halipewi kipaumbele. Hata hivyo, hii imefanya kukiuka sheria na taratibu za kiutendaji kwa vile si haki kuwatendea wateja wetu namna tunavyowatendea. 

Na kwa mazingira hayo wakati mwingine tumeukosa ukweli kutoka kwa watoto kwani hukosa amani kwa mazingira wanayohojiwa au kutakiwa kutoa taarifa” alisisitiza Nyamara.
Changamoto nyingine alizitaja kuwa ni kuongezeka kwa matukio ya ukatili dhidi ya watoto na watoto wenyewe kujihusisha kwenye matukio makubwa ya ukiukwaji wa sheria za nchi. 

Aliongeza kuwa jamii kushindwa kutoa ushirikiano kwenye masuala ya ulinzi na usalama wa mtoto kwa kuogopa kuitwa mahakamani. Pia kushindwa kufanikiwa kwa mashauti ya watoto katika baadhi ya halmashauri.

Ofisi ya mkuu wa mkoa wa Iringa iliandaa kikao cha uhamasishaji shughuli za ustawi wa jamii kwa kamati ya ulinzi na usalama ya mkoa, wataalam ofisi hiyo na Halmashauri ili kuwajengea uelewa wa masuala ya ulinzi wa mtoto.
=30=

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Habari zinazoendelea hivi sasa

SERIKALI KUWEZESHA VIJANA KUKOPA

Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa Serikali itaendelea kuwawezesha vijana kwa kuwatengenezea mazingira mazuri ya mikopo ili waweze k...