Jumanne, 18 Machi 2014

WADAU WA MAPAMBAYO YA UKIMWI WAUNGANISHE NGUVU



Na. OFISI YA MKUU WA MKOA

SERIKALI mkoani Iringa imewataka wadau wanaojihusisha na mapambano dhidi ya ukimwi kuunganisha nguvu zao na kupambana na maambukizi mapya ya virusi vya ukimwi hasa kwa wanawake na wasichana mkoani Iringa.

Kauli hiyo imetolewa na Katibu Tawala Mkoa wa Iringa, Wamoja Ayubu alipokuwa akifungua mkutano wa kujadili matokeo ya utafiti wa hali ya maambukizi ya virusi vya ukimwi mkoa wa Iringa uliofanyika katika ukumbi wa Wilolesi Hiltop hoteli mjini Iringa.

Wamoja amesema “Kwa mujibu wa Utafiti dhidi ya viashiria vya maambukizi ya virusi vya UKIMWI na Malaria uliofanyika mwaka 2012 unaonesha kuwa maambukizi ya virusi vya UKIMWI katika Mkoa wa Iringa ni asilimia 9.1 ukiwa unashika nafasi ya pili nyuma ya Mkoa wa Njombe. Kiwango hiki ni kikubwa kikilinganishwa na wastani wa maambukizi ya virusi vya UKIMWI kitaifa ambao ni wastani wa asilimia 5.1”.

Amesema kuwa katika mkoa wa Iringa, wanawake ndilo kundi linalobeba mzigo mkubwa kutokana na tatizo la maambukizi ya virusi vya ukimwi na ukimwi iliwa kuadhirika zaidi kuliko wanaume. Amesema kuwa takwimu zinaonesha kuwa wanawake wameathirika kwa asilimia 11 ikilinganishwa na wanaume ambao wameathirika kwa asilimia 6.9. amesema kwa mujibu wa takwimu hizo, wanawake ni wahanga kwa asilimia 4.1 zaidi ya wanaume.

Wamoja amesema kuwa changamoto hiyo ya kijinsia haijaishia kwa wanawake bali imeendelea hadi katika kundi la vijana wa kike wenye umri kati ya miaka 15-24. Amesema kundi hilo la  wasichana ndiyo wameathirika zaidi na ugonjwa wa ukimwi ikiwa ni asilimia saba (7) ikilinganishwa na asilimia 1.5 ya wavulana. Amesema kuwa matokeo ya utafiti huo yatakayojadiliwa siku hiyo yatasaidia kufafanua tatizo hilo kwa undani na kutoa nafasi pana ya mjadala wa tatizo husika.

Katibu Tawala Mkoa wa Iringa amewataka wajumbe wa mkutano huo kujikita katika maeneo ya kimkakati yafuatayo. Maeneo hayo ameyataja kuwa ni kutambua na kuainisha sababu za kijamii, kitamaduni na mila zinazochangia katika kuongezeka kwa maambukizi mapya ya virusi vya ukimwi. Maeneo mengine ni kujipanga kuhakikisha mnayafikia makundi yaliyo katika hatari kubwa ya kupata maambukizi ya virusi vya ukimwi hasa wanawake na wasichana wanaofanya kazi za kubadili ngono kwa pesa.

Maeneo mengine ni kuelezea mipango ya mawasiliano kuhusu mabadiliko ya tabia zenye ufanisi na kuboresha rufaa pamoja na ushiriki na upimaji wa virusi vya ukimwi, tiba na matunzo kwa wenye virusi vya ukimwi na ukimwi. Eneo lingine amelitaja kuwa ni upokeaji na ubora wa huduma ya tohara ya hiari ya kitibabu kwa wanaume kwa lengo la kujikinga na maambukizi ya virusi vya ukimwi na kupunguza kasi ya kuenea kwa maambukizi mapya.

Mkutano wa kuwasilisha taarifa ya utafiti wa kuzuia maambukizi ya virusi vya ukimwi ujulikaoa kama R2P uliofanyika mjini Iringa umehudhuriwa na wadau mbalimbali wakiwemo watafiti, wanazuoni na taasisi mbalimbali zikiwemo mpango wa Taifa wa kudhibiti ukimwi, tume ya taifa ya kudhibiti ukimwi, USAID, REPFAR, kituo cha kudhibiti magonjwa, idara ya ulinzi, vyuo vikuu vya Johns Hopkins, Tulane na Muhimbili. Taasisi nyingine ni Jhpiego, AMREF, FHI/360, PSI, Tunajali, Engender health, Africare, TCCP, JSI na UNICEF.
=30=




Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Habari zinazoendelea hivi sasa

SERIKALI KUWEZESHA VIJANA KUKOPA

Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa Serikali itaendelea kuwawezesha vijana kwa kuwatengenezea mazingira mazuri ya mikopo ili waweze k...