Jumamosi, 14 Juni 2014

HALI YA UCHANGIAJI DAMU NYANDA ZA JUU KUSINI



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Maadhimisho ya siku ya wachangia damu duniani yanalenga kuongeza uelewa kwa wananchi kuhusu umuhimu wa kuchangia damu kwa hiari pamoja na kuwatambua na kuwaenzi wachangia damu wa hiari.
Meneja wa Mpango wa Taifa wa Damu Salama Nyanda za Juu Kusini
 Kauli hiyo imetolwa na Meneja wa Mpango wa Taifa wa Damu Salama kanda ya nyanda za juu kusini, Dkt. Kokuhaba Mukurasi alipokuwa akifafanua umuhimu wa maadhimisho ya siku ya wachangia damu duniani maadhimisho yaliyofanyika ngazi ya kanda katika mkoa wa Iringa.
Amesema kuwa maadhimisho hayo yanalenga kuongeza uelewa kwa wananchi kuhusu umuhimu wa kuchangia damu kwa hiari na kuwatambua, kuwaenzi na kuwashukuru wachangia damu kwa hiari mara kwa mara bila ya malipo yoyote.
Dkt. Mukurasi amesema kuwa maadhimisho ya siku ya wachangia damu duniani mwaka 2014 yanaongozwa na kaulimbiu isemayo “damu salama uhai wa mama”. Amesema kaulimbiu hiyo ni muhimu kutokana na ukweli kuwa zaidi ya asilimia 30 ya damu salama hutumiwa na akina mama wajawazito wanapopata matatizo ya uzazi ikiwa ni pamoja na kutoka damu nyingi kabla na baada ya kujifungua, mama anapofanyiwa upasuaji na mimba inapotoka.
Meneja wa kanda amesema kuwa mama na mtoto hutumia zaidi ya asilimia 80 ya tiba ya damu salama hivyo mahitaji hayo yanaonesha umuhimu wa kuwepo kwa uhakika wa damu salama katika hifadhi ya damu.
Akiongelea mahitaji ya damu salama kwa kanda ya nyanda za juu kusini, Meneja wa Taifa wa Mpango wa Damu Salama amesema kuwa kanda hiyo inahitaji wastani wa chupa za damu 28,000 kwa mwaka. Amesema kuwa kanda hiyo hukusanya wastani wa chupa 19,331 kwa mwaka ikiwa ni wastani wa asilimia 70 tu na kuelezea kuwa uhitaji bado ni mkubwa.
Mwakilishi wa Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Gerald Guninita
 Akitoa shukrani kwa makundi mbalimbali ya kijamii, Gerald Guninita aliyemuwakisha mkuu wa mkoa wa Iringa ameyapongeza makundi yote ya kijamii, kidini, wanafunzi na wananchi wa mkoa wa Iringa waliojitolea damu kwa hiari mara kwa mara. Amesema kuwa damu inayokusanywa na Mpango wa Taifa wa Damu Salama hutolewa bila malipo katika vituo vinavyotoa tiba ya damu.
=30=


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Habari zinazoendelea hivi sasa

SERIKALI KUWEZESHA VIJANA KUKOPA

Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa Serikali itaendelea kuwawezesha vijana kwa kuwatengenezea mazingira mazuri ya mikopo ili waweze k...