Jumatano, 18 Juni 2014

IRINGA WAASWA KUTONYANYASA WATOTO



Na. Dajali Mgidange, IRINGA
Wananchi wa manispaa ya Iringa wameaswa kutokuwatumikisha watoto katika ajira mbaya na unyanyasaji wa aina yoyote ili watoto waweze kuishi katika amani na ukuaji stahiki.
Mstahiki Meya wa Manispaa ya Iringa, Amani Mwamwindi
 Kauli hiyo imetolewa na mstahiki Meya wa Manispaa ya Iringa Amani Mwamwindi alipokuwa akizungumza na wananchi wa manispaa ya Iringa na watoto waliojitokeza katika maadhimisho ya siku ya mtoto wa Afrika yaliyofanyika katika uwanja wa Mwembetogwa uliopo kata ya Makorongoni manispaa ya Iringa.             
Mwamwindi amewataka wananchi wa manispaa ya Iringa kupinga utumikishaji wa watoto katika ajira mbaya na hatarishi. Maeneo mengine hatarishi ameyataja kuwa ni mauaji ya albino, ubakaji, ulawiti, vipigo na wazazi kutelekeza watoto wao.
“Maadhimisho haya hufanyika kila mwaka kwa lengo la kuikumbusha jamii haki za watoto. Tukio hili ni kubwa lina umuhimu wake katika manispaa yetu, Taifa na Kimataifa tukio hili ni kumbukumbu ya watoto wapatao 15,000 waliouwawa na makaburu huko Soweto Afrika Kusini tarehe 16/06/1976 wakipinga maamuzi ya serikali hiyo kuwafundisha watoto lugha ya kikaburu” alisema Mwamwindi.

Akiongelea kaulimbiu ya maadhimisho isemayo kupata elimu bora isiyo na vikwazo ni haki ya kila mtoto, Meya amesema kuwa kaulimbiu hiyo imesisitiza
wazazi, walezi, familia, serikali na wadau mbalimbali wanaojishughulisha na shughuli za maendeleo ya watoto kwa kuliangalia kundi hili, kuhakikisha wanapata haki zao za msingi za kupata elimu bila vikwazo kwa msingi kwamba mtoto awapo shuleni hatakiwi kunyanyaswa kwasababu haki yake yeye ni kusoma na kupata Elimu. Amesema kuwa masuala ya ada, michango mbalimbali ni jukumu la mzazi au mlezi. Amesema kuwa kumekuwepo na tabia ya baadhi ya watoto kurudishwa nyumbani kwa kisingizio cha kutokumaliza ada na baadhi ya michango  na kusisitiza kuwa jukumu hilo ni la mzazi.

Regina Mushi ambaye ni mzazi alisema siku ya mtoto  wa Afrika ni siku nzuri kwa watoto kwa sababu imeweza kuwakutanisha pamoja na kujadili changamoto zinazowakabili. Amesema kuwa imekuwepo changamoto ya baadhi ya wazazi/ walezi kuwafungia watoto ndani na mwingine aliweza kumfungia mtoto kwenye boksi na hatimae baadae kufariki.
Mtoto Henry Mwalongo amesema “siku ya mtoto wa Afrika inawahimiza wazazi kutowanyanyasa watoto hasa katika swala la elimu kutupatia elimu isiyo na vikwazo vya aina yoyote ile”.
Siku ya mtoto wa Afrika kuadhimishwa tarehe 16 Juni kila mwaka barani Afrika kufuatia mauaji ya watoto zaidi ya 15,000 huko Soweto Afrika Kusini.
=30=

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Habari zinazoendelea hivi sasa

SERIKALI KUWEZESHA VIJANA KUKOPA

Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa Serikali itaendelea kuwawezesha vijana kwa kuwatengenezea mazingira mazuri ya mikopo ili waweze k...