Jumamosi, 14 Juni 2014

HOSPITALI YA RUFAA YA MKOA...



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Serikali itaendelea kutengeneza mazingira mazuri ya ushirikiano na wadau wa maendeleo kwa lengo la kuwahakikishia huduma bora za matibabu wananchi wa Iringa.
Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma (kulia) na mwakilishi wa hospitali ya Vicenza Dkt. Oscar Banzato
Kauli hiyo imetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma alipokuwa akipokea vifaa tiba vilivyotolewa kwa msaada na hospitali ya Vicenza ya nchini Italia katika hospitali ya rufaa ya Iringa.
Dkt. Ishengoma amesema kuwa serikali itaendelea kutengeneza na kuimarisha mazingira mazuri ya kuwezesha ushirikiano na wadau wa maendeleo kwa manufaa ya wananchi wa mkoa wa Iringa na taifa kwa ujumla. Amesema kuwa ni matumaini yake kuwa ushirikiano huo utaendelea kuimarishwa na kudumishwa ili uweze kunufaisha wananchi wengi.
Mwakilishi wa hospitali ya Vicenza toka nchini Italia Dkt. Oscar Banzato ameihakikishia serikali kuwa ushirikiano baina ya Italia na hospitali ya Vicenza utaendela kuimarishwa ili kuiwezesha hospitali ya rufaa ya mkoa wa Iringa kutoa tiba kwa urahisi kwa wananchi wa mkoa wa Iringa na wengine watakaopita katika hospitali hiyo.
Dkt. Oscar Banzato
 Katika taarifa ya hospitali ya rufaa ya mkoa wa Iringa iliyowsilishwa mganga mfawidhi Dkt. Deogratius Manyama amesema kuwa mkataba wa kwanza wa ushirikiano baina ya hospitali ya rufaa ya mkoa wa Iringa na hospitali ya Vicenza ya mkoa wa Veneto nchini Italia ulisainiwa mwezi Oktoba, 2006. Amesema kuwa mkataba huo uliokuwa na thamani ya Euro 985,000 ulilenga uboreshaji wa ubora wa utoaji wa huduma za afya zinazotolewa kwa wakazi wa mkoa wa Iringa. Amevitaja vipengele vya mkataba huo kuwa ni kuboresha miundombinu ya hospitali ya rufaa ya mkoa. Vipengele vingine amevitaja kuwa ni kuisaidia hospitali ya rufaa ya mkoa kupata vifaa vya kisasa na kutoa msaada wa kitaalamu kwa hospitali ili kuboresha ubora wa huduma.
Akiongelea utekelezaji huo, Dkt. Manyama amesema kuwa hospitali ya Vicenza tayari imekamilisha ujenzi wa jengo la kujifungulia wajawazito ambalo limeanza kutumika tangu mwezi Agosti, 2011. Ameongeza kuwa ujenzi wa wodi ya watoto pia umekamilika na kuanza kutumika tangu mwezi Septemba, 2013.
=30=

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Habari zinazoendelea hivi sasa

SERIKALI KUWEZESHA VIJANA KUKOPA

Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa Serikali itaendelea kuwawezesha vijana kwa kuwatengenezea mazingira mazuri ya mikopo ili waweze k...