Jumatano, 4 Juni 2014

IRINGA WATAKIWA KUTUNZA MAZINGIRA



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Wananchi mkoani Iringa wametakiwa kutunza mazingira na kusimamia sheria zilizopo kwa lengo la kuhakikisha vyanzo vya maji vinalindwa.

Kauli hiyo imetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma alipokuwa akizindua jumuiya ya watumia maji wa bonde dogo la mto Mfyamba katika kijiji cha Sadani wilayani Mufindi.

Dkt. Ishengoma amesema “kila mmoja wetu ni shahidi wa uharibifu wa mazingira katika mto wetu, ninapenda kuwakumbusha kuwa ni jukumu letu sote kutunza na kuhifadhi mazingira na kubadilisha hali hiyo kwa kuacha kuchepusha maji kinyume na sheria, kuchimba mchanga na mawe jirani na mto na katika vyanzo vyingine vya maji vinavyoingia katika mto Mfyamba na kusababisha uchafuzi wa maji hivyo kuhatarisha afya za binadamu na viumbe walioko majini”. 

Aidha, amewataka wananchi kuacha kilimo cha kiangazi kiitwacho vinyungu kando kando ya mto na vyanzo vingine vinavyoingiza maji katika mto Mfyamba, ukataji ovyo wa miti rafiki na maji na shughuli za uchimbaji wa madini mahususi katika kijiji cha Ihanzutwa.

Akiongelea umuhimu wa mto Mfyamba, Mkuu wa Mkoa wa Iringa amesema kuwa shughuli nyingi za kujipatia kipato na chakula katika eneo linalozunguka mto huo hutegemea sana uwepo wa mto huo. Amesema kuwa mto huo utakapoharibiwa utahatarisha upatikanaji wa maji na afya za wananchi wanaotumia maji yam to huo.

Akionesha msisitizo, Dkt. Ishengoma amepiga marufuku shughuli zote za kibinadamu kama ufyatuaji tofali, kilimo cha bustani, ufugaji holela, uoshaji wa magari na utupaji taka katika au kando kando ya vyanzo vya maji.

Afisa wa bonde la Rufiji, Idris Msuya amesema kuwa kuundwa kwa vyama vya watumia maji ni hatua za utekelezaji sera ya maji ya mwaka 2002 inayosisitiza ushirikishwaji wa watumia maji katika mipango ya usimamizi wa rasilimali za maji. 
Amesema kuwa kuundwa kwa jumuiya ya watumia maji bonde dogo la mto Mfyamba ni hatua muhimu katika utekelezaji wa sera ya maji. Ameutaka uongozi wa wilaya kuwa karibu na jumuiya hiyo katika utekelezaji wa majukumu yake.

Akiongelea tatizo la kukauka kwa mto Ruaha wakati wa kiangazi na kusababisha matatizo ya uzalishaji wa umeme katika bwawa la Mtera na Kidatu, Afisa wa bonde la Rufiji amesema “hili ni tatizo la kitaifa na tunastahili kulichukua hilimaanani kwani mto Mfyamba ni tawi la mto Ndembera ambao ni tawi la muhimu la mto Ruaha Mkuu”. Amesema kutokana na hali hiyo mchango wa wadau wote katika kuimarisha mtiririko wa maji katika mto Ruaha mkuu ni wa muhimu sana na jamii mzima inastahili kuchukua hatua ili kuondoa tatizo hilo. Amesema kuwa kukauka kwa mto wowote ni dalili ya matumizi mabaya ya maji katika baadhi ya maeneo, ufanisi mdogo wa miundombinu ya umwagiliaji katika maeneo hayo na uharibifu wa mazingira na vyanzo vya maji.

Bonde dogo la mto Mfyamba limeenea katika wilaya za Mufindi na Mbarali.
=30=

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Habari zinazoendelea hivi sasa

SERIKALI KUWEZESHA VIJANA KUKOPA

Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa Serikali itaendelea kuwawezesha vijana kwa kuwatengenezea mazingira mazuri ya mikopo ili waweze k...