Jumatano, 4 Juni 2014

WAWEKEZAJI WAJITOKEZE ZAIDI KUWEKEZA KATIKA KILIMO CHA MBEGU BORA



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Serikali imetoa rai kwa wawekezaji zaidi kujitokeza katika uzalishaji wa mbegu bora ili kuinua kilimo na kukuza uchumi nchini.

Kauli hiyo imetolewa na Naibu Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika Godfrey Zambi katika hotuba yake wakati wa hafla fupi ya makabidhiano ya shamba la kuzalisha mbegu la Dabaga baina ya Wakala wa kuzalisha mbegu na wakfu wa Clinton katika kijiji cha Lukani wilayani Kilolo.
Naibu Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Godfrey Zambi katikati

Zambi amesema “tunaalika wawekezaji wengi zaidi katika uwekezaji wa kilimo cha mbegu bora nchini”. Amesema kuwa dhumuni kuu ni uzalishaji wa mbegu bora kwa kiwango kikubwa ili wananchi wengi waweze kunufaika na upatikanaji wa mbegu bora nchini. Amesema kuwa serikali inavutia uwekezaji katika kilimo cha uzalishaji wa mbegu kutokana na ukweli kuwa uzalishaji wa mbegu nchini bado upo chini sambamba na matumizi ya mbegu bora. Amesema kuwa katika kuhakikisha nchi inakuwa na mbegu bora na za kutosha kwa ajili ya wakulima serikali inaendelea kujenga uwezo ikiwa ni pamoja na kuishirikisha sekta binafsi.

Akiongelea faida wa shamba la kuzalisha mbegu la Dabaga, naibu waziri amesema kuwa shamba hilo ni muhumu kwa lengo la kupata mbegu kwa bei rahisi. Faifanyingine ameitaja kuwa ni upatikanaji wa ajira ya moja kwa moja na ajira ya muda kwa wananchi na wakulima wanaozunguka eneo la shamba hilo. Amesema kuwa wananchi watapata fursa ya kujifunza juu ya uzalishaji wa mbegu bora katika shamba hilo.

Akiongelea majukumu ya wakala wa kuzalisha mbegu nchini, Afisa mtendaji mkuu wa wakala wa kuzalisha mbegu nchini Dkt. Firmin Mizambwa amesema kuwa wakala wanajukumu la kuongeza uzalishaji wa mbegu bora kwa wakulima. Jukumu linguine amelitaja kuwa ni kuhamasisha ushiriki wa sekta binafsi katika uzalishaji wa mbegu bora pamoja na kuongeza ajira kwa wananchi wanaozunguka maeneo ya mashamba ya wakala hiyo. Amesema kuwa kutokana na wakulima wengi kutotumia mbegu bora nchini, wakala wa mbegu unajukumu la kuhamasisha matumizi ya mbegu bora nchini pamoja na kushirikiana na vituo vya utafiti.

Katika salamu za kaimu katibu tawala mkoa wa Iringa, Kilasi Mwakilasi amesema kuwa ushirikiano baina ya serikali na sekta binafsi ni fursa muhimu kwa mkoa wa Iringa na wananchi wake. Amesema ushirikiano huo unajikita katika maeneo mbalimbali yakiwa ni pamoja na utaalamu, mafunzo na kuongeza fursa ya ajira. 

Amesema kutokana na mkoa wa Iringa kuwa mzalishaji mkubwa wa mahindi na alizeti ushirikiano huo utachangia katika kukuza uzalishaji wa mazao hayo. Amesema kuwa mkoa wa Iringa utaendelea kutoa ushirikiano kwa sekta binafsi kwa manufaa ya wananchi wa mkoa na taifa kwa ujumla.

Shamba la kuzalisha mbegu bora la Dabaga linaukubwa wa Hekta 1058.
=30=

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Habari zinazoendelea hivi sasa

SERIKALI KUWEZESHA VIJANA KUKOPA

Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa Serikali itaendelea kuwawezesha vijana kwa kuwatengenezea mazingira mazuri ya mikopo ili waweze k...