Jumanne, 10 Juni 2014

MAADHIMISHO YA SIKU YA WACHANGIA DAMU DUNIANI KANDA YA NYANDA ZA JUU KUSINI



TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI KUHUSU MAADHIMISHO YA SIKU YA WACHANGIA DAMU DUNIANI TAREHE 01 HADI 14 JUNI, 2014 ILIYOTOLEWA NA MKUU WA MKOA WA IRINGA OFISINI KWAKE TAREHE 09/06/2014

Ndugu Wananchi,
Tanzania itaadhimisha kilele cha siku ya wachangia Damu duniani tarehe 14 Juni, 2014 Kitaifa Mkoani Kigoma.

Ndugu Wananchi,
Kauli mbiu ya mwaka huu ambayo inaenda sambamba na miaka 11 tangu siku ya wachangia damu ilipoanzishwa ni “DAMU SALAMA  UHAI WA MAMA” (SAFE BLOOD FOR SAVING MOTHERS).

Ndugu Wananchi,
Mkoa wa Iringa mwaka huu umebahatika kuwa mwenyeji wa Maadhimisho ya Siku ya wachangia Damu duniani Kikanda kuanzia tarehe 1 Juni hadi tarehe 14 Juni, 2014 Siku ya Kilele itakayofanyika  katika viwanja vya Mwembetogwa katika Manispaa ya Iringa.



Ndugu Wananchi,
Madhumuni ya siku hii ni kuongeza uelewa kwa wananchi kuhusu umuhimu wa kuchangia damu kwa hiari pia kuwatambua, kuwaenzi na kuwashukuru wachangia damu ambao wamekuwa wakichangia damu kwa hiari mara kwa mara bila malipo yoyote.

Ndugu Wananchi,
Damu ni uhai, hivyo kila binadamu mwenye ubinadamu na utu anayo nafasi ya kutoa damu yake ambayo ni uhai kwa wahitaji wa tiba ya damu.

Ndugu Wananchi,
Vifo vingine vya akina mama katika Hospitali zetu husababishwa na ukosefu wa damu iliyo salama. Hivyo kila mtu anaguswa kwani hakuna asiyezaliwa na mama. Na ni nani kama mama?

Ndugu Wananchi,
Kwanini kauli mbiu hii ya “uchangiaji damu ni uhai wa mama” imetolewa mwaka huu?
Ukweli ni kwamba zaidi ya asilimia 30 ya damu salama hutumiwa na akina mama wajawazito hasa wanapo pata matatizo mbalimbali ya uzazi kama kutokwa na damu nyingi kabla au baada ya kujifungua, mimba inapotoka  au mama anapofanyiwa upasuaji.

Ndugu Wananchi,
Damu ni uhai na ina thamani kubwa, Damu inaweza kuhifadhiwa kwa muda wa siku 35 tu kabla ya muda wake wa kutumika kwisha. Hivyo zoezi la kuchangia damu ni endelevu na la kudumu, chupa moja ya damu inaweza kuokoa maisha ya watu zaidi ya mmoja kama ikigawanywa kitaalamu kwenye mazao mbalimbali za damu kama vile plasma, chembe sahani na chembe nyekundu.

Ndugu Wananchi,
Huduma ya damu salama huokoa maisha ya mamilioni ya watu kila mwaka duniani. Aidha, upatikanaji wa damu kwa wakati huongeza nafasi ya kuishi kwa wahitaji wa damu,

Ndugu Wananchi,
Kwa kifupi nitayataja makundi ya watu ambao huitaji damu na asilimia zake kama ifuatavyo:
·        Watoto wadogo hasa walio chini ya umri wa miaka mitano (50%)
·        Wajawazito na wanawake wenye matatizo ya uzazi (30%)
·        Majeruhi wa ajali mbalimbali hasa ajali za barabarani na watu wanaofanyiwa tiba ya upasuaji (15%)
·        Wale wote wenye magonjwa mbalimbali yanayosababisha upungufu wa damu (5%)

Ndugu Wananchi,
Katika nchi yetu na kanda yetu mahitaji ya damu yanazidi upatikanaji wake, Mpango wa Taifa wa Damu Salama unakabiliwa na changamoto ya kuhakikisha kunakuwepo na upatikanaji wa damu salama na ya kutosha ili kuweza kuwasaidia wagonjwa wanaohitaji damu hospitalini.

Ndugu Wananchi,
Mahitaji ya damu Kitaifa ni wastani wa chupa 400,000-450,000 Mpango wa Taifa wa Damu Salama unakusanya wastani wa chupa 100,000-120,000 kwa mwaka.
Kikanda mahitaji ni wastani wa chupa za damu 28,000 ambapo Kanda ya Nyanda za Kusini huweza kukusanya jumla ya chupa 19,331 ambayo ni sawa na asilimia 70 tu, hivyo tunakabiliwa na upungufu mkubwa wa Damu Salama.

Ndugu Wananchi,
Uchangiaji damu wa hiari wa bila malipo na wa mara kwa mara ni msingi wa upatikanaji wa damu salama na ya kutosha. Wachangiaji damu wa kujirudia ni salama kwani damu yao ina kiasi kidogo cha maambukizo ya magonjwa yanayoweza kuenezwa kwa njia ya damu.
Natoa rai kwa Wakazi wa Mkoa wa Iringa na Watanzania wote kwa ujumla kujenga utamaduni wa kuchangia damu kwa hiari mara kwa mara ili Kanda yetu iwe na akiba ya damu ya kutosha.

Ndugu Wananchi,
Iwapo asilimia moja ya Wakazi wa Kanda hii wakiamua kuwa wachangiaji damu wa kujirudia Mpango wa Taifa wa Damu Salama utaweza kukidhi mahitaji ya damu katika Hospitali zetu.

Ndugu Wananchi,
Damu Salama inatolewa bure katika vituo vyote vya kutolea huduma kama mwananchi akiambiwa alipie damu atoe taarifa kwa uongozi na ikibanika kweli mtumishi aliyefanya hivyo atachukuliwa hatua za kinidhamu za kiutumishi.

Ndugu Wananchi,
Mkoa wa Iringa umejiwekea mkakati wa kupunguza vifo vya uzazi na mtoto kupitia mpango wa uwajibikaji katika kupunguza vifo hivyo na moja ya kipaumbele ni uanzishwaji wa kituo kidogo cha kuchangia damu salama (Blood Collection Satellite Site) Mkoani ambacho gharama yake ni Tshs. 140,000,000.00.

Hivyo, nawaomba wadau na watu wote wenye mapenzi mema kuchangia kuanzishwa kwa kituo hicho kurahisisha upatikanaji wa damu salama kwa wakati na kuokoa maisha ya akina mama na watoto.

Ndugu Wananchi,
NAMALIZIA KWA KUSEMA NAWAOMBA WANANCHI MJITOKEZE KWA WINGI KATIKA SIKU HIZO ZA MADHIMISHO ILI TUONYESHE MSHIKAMANO NA KUCHANGIA  DAMU AMBAYO NI UHAI KWA MAMA.

KAULI MBIU: DAMU SALAMA UHAI WA MAMA


ASANTENI KWA KUNISIKILIZA

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Habari zinazoendelea hivi sasa

SERIKALI KUWEZESHA VIJANA KUKOPA

Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa Serikali itaendelea kuwawezesha vijana kwa kuwatengenezea mazingira mazuri ya mikopo ili waweze k...