Jumapili, 29 Juni 2014

RC IRINGA AKWEPA ZAIDI YA MARA 3 JUKWAANI



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Mkuu wa mkoa wa Iringa Dkt. Christine Ishengoma ameweka rekondi nyingine katika mikesha ya mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka 2014.
Kauli hiyo imetolewa na kiongozi wa wakimbiza Mwenge wa Uhuru kitaifa Rachel Kassanda katika kijiji cha Idofi mkoani Njombe wakati akiwaaga wananchi wa mkoa wa Iringa baada ya kukamilisha mbio hizo za siku nne mkoani Iringa.
Kassanda amesema kuwa tokea Mwenge wa Uhuru umewashwa katika uwanja wa Kaitaba tarehe 2/5/2014 mkuu wa mkoa wa Iringa ameweza kushiriki katika mikesha mitatu mfululizo. Amesema kuwa katika mikoa yote minane iliyopitiwa na Mwenge wa Uhuru mwaka 2014, Dkt. Ishengoma ameonesha kitendo cha kipekee kilichopelekea hamasa kwa wananchi kujitokeza na kushiriki katika mikesha ya Mwenge wa Uhuru. Amesema kuwa kitendo hiki cha kizalengo hakina budi kuigwa ili kuongeza hamasa katika mikesha ya Mwenge wa Uhuru.
Akiongelea miradi ya maendeleo na thamani ya fedha katika miradi hiyo, Kassanda amesema kuwa mkoa wa Iringa umeitendea haki miradi ya maendeleo ikilinganishwa na thamani ya fedha iliyotumika. Amesema ushirikiano uliyopo baina na viongozi na watendaji ni chachu katika kufanikisha miradi ya maendeleo kwa lengo la kutoa huduma bora kwa wananchi.
Kiongozi huyo wa wakimbiza Mwenge wa Uhuru kitaifa amewataka watumishi wa umma kusimama katika nafasi zao kuhakikisha wanatenda haki na wajibu wao kwa wananchi na serikali yao. Amesema kuwa mtumishi wa umma ni kioo cha wananchi na kuwataka watumie nafasi wazopewa kuwahudumia wananchi kwa haki. Amesema kuwa sifa ya mtumishi ni utoaji huduma kwa haki. Amewataka kuepuka vitendo vyote na mazingira yanayotengeneza mianya ya rushwa. Amesema kuwa rushwa inafifisha haki na kumfanya mwenye haki kudhulumiwa haki yake.
Kiongozi wa wakimbiza Mwenge wa Uhuru kitaifa amesema kuwa kila mwaka mbio za Mwenge wa Uhuru hubeba ujumbe maalum ambao unawajulisha na kuwatambulisha wananchi masuala makuu yanayolikabili taifa kwa wakati huo. Amesema kuwa mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka 2014 zimebeba ujumbe usemao “Katiba ni sheria kuu ya nchi” wenye kaulimbiu ‘jitokeze kupiga kura ya maoni tupate katiba mpya’. Amesema kuwa ujumbe una lenga kuwahamasisha wananchi kujitokeza na kushiriki  kupiga kura ya maoni ili kupata Katiba mpya kwa mustakabali wa Taifa.
Iringa ni mkoa wa tisa kutembelewa na Mwenge wa Uhuru mwaka 2014. Mikoa iliyotangulia ni Kagera, Kigoma, Katavi, Rukwa, Mbeya, Singida, Dodoma na Morogoro. Ukitokea Iringa mkoani Iringa Mwenge wa Uhuru utakimbizwa katika mkoa wa Njombe katika halmashauri tano.
=30=

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Habari zinazoendelea hivi sasa

SERIKALI KUWEZESHA VIJANA KUKOPA

Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa Serikali itaendelea kuwawezesha vijana kwa kuwatengenezea mazingira mazuri ya mikopo ili waweze k...