Jumapili, 10 Agosti 2014

IRINGA INAFURSA NYINGI ZA UWEKEZAJI



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa - IRINGA
Mkoa wa Iringa umejaaliwa fursa nyingi za uwekezaji ambazo zikitumika vizuri zitasaidia kuinua pato la mwananchi na Taifa kwa ujumla.
Kauli hiyo imetolewa na Mwenyekiti wa Baraza la Biashara la Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma katika hotuba yake ya ufunguzi wa Baraza la Biashara la Mkoa wa Iringa lililofanyika katika ukumbi wa mikutano wa VETA uliopo Manispaa ya Iringa.
Baraza la Biashara la Mkoa wa Iringa
Dkt. Ishengoma amesema “Mkoa wa Iringa una fursa nyingi za uwekezaji kama tutazitumia vizuri zinaweza kusaidia kukuza pato la mwananchi na Taifa kwa ujumla. Kuna fursa katika utalii, viwanda, biashara, kilimo, kilimo cha maua, matunda, ufugaji, misitu na huduma za jamii”. Amesema “ni jukumu letu sisi kuziainisha fursa hizi na kufanya uwekezaji kwa wawekezaji wa ndani na nje ya nchi”. Amesema kuwa Mkoa wa Iringa ulishafungua milango kwa wawekezaji wa ndani na nje kuja kuwekeza. Amesema kuwa Mkoa umejitahidi kuboresha mazingira na miundombinu ya uwekezaji ila zoezi hilo linakabiliwa na changamoto ya kuzitangaza fursa hizo ili zieleweke na kuvutia wawekezaji.
Dkt. Ishengoma ambaye pia ni Mkuu wa Mkoa wa Iringa amekitumia kikao hicho kuwapongeza wawekezaji ambao wamekwisha zitambua fursa zilizopo za uwekezaji na kuzitumia na kutoa wito kwa wawekezaji wengine kufuata mfano huo. Aidha, ameziagiza Halmashauri za Mkoa wa Iringa kuwasaidia wawekezaji wanapojitokeza kuwekeza Iringa. Amezitaka Halmashauri kuwa msaada kwa wawekezaji badala ya kuwa kikwazo. Amepongeza juhudi za wawekezaji wanaowekeza katika hoteli za kitalii kwa lengo la kusaidia kuinua sekta ya utalii mkoani Iringa.
Dkt. Ishengoma amesema kuwa Taifa limeandaa mkakati wa kukuza uchumi na kupunguza umasikini awamu ya pili (2011-2015) unaolenga kufikia Dira ya Taifa ya maendeleo ya mwaka 2025. Amesema kuwa mkukuta umejengwa katika nguzo tatu na kuzitaja kuwa ni kuhamasisha ubora wa maisha ya watu na ustawi wa jamii. Nguzo nyingine ni ukuaji wa uchumi na kupunguza umasikini wa kipato na utawala bora na uwajibikaji. Amesema kuwa kufanikiwa kwa malengo ya mkukuta kunategemea ushiriki wa wadau wote katika utekelezaji wake. 
 =30=

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Habari zinazoendelea hivi sasa

SERIKALI KUWEZESHA VIJANA KUKOPA

Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa Serikali itaendelea kuwawezesha vijana kwa kuwatengenezea mazingira mazuri ya mikopo ili waweze k...