Jumanne, 5 Agosti 2014

NJK WATAKIWA KUBUNI MKAKATI WA KUJITANGAZA...



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa- IRINGA
Wadau wa masuala ya kilimo wa mikoa ya Nyanda za Juu Kusini wametakiwa kubuni mkakati wa kijitangaza ili shughuli zao hazifahamiki kwa watu wengi zaidi.
Kauli hiyo imetolewa na mgeni rasmi wakati wa kukagua mabanda ya maonesho Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma wakati wa majumuisho baada ya kutembelea mabanda ya maonesho ya Nanenane katika uwanja wa maonesho wa John Mwakangale jijini Mbeya.
Mkuu wa Mkoa wa Iringa, dkt. Christine Ishengoma (Mb.) kushoto na mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya ya Mufindi Nuhu Mwasumilwe (kulia)
Dkt. Ishengoma amesema kuwa mikoa ya Nyanda za Juu Kusini imepiga hatua kubwa sana katika matumizi ya teknolojia ya habari na mawasiliano (Tehama) lakini shughuli hizo hazitangazwi. Amesema kuwa vyuo vikuu vinafanya kazi nzuri katika matumizi ya Tehama katika kubuni na kutengeneza nafasi za kazi. Amesema kuwa ubunifu huo ni mzuri hasa katika kuwasaidia vijana kujiajiri na kupunguza tatizo la ajira kwa vijana nchini. Amesema kuwa teknolojia zinazobuniwa na vyuo vikuu zitangazwe na kusambazwa kwa mujibu wa taratibu.
Mkuu wa Mkoa wa Iringa amewataka wakazi wa mikoa ya Nyanda za Juu Kusini kujikita katika kilimo cha mbogamboga, matunda na maua. Ameshauri matumizi ya “greenhouse” kwa sababu mkulima anaweza kulima kilimo cha mbogamboga na matunda katika eneo dogo kwa ufanisi na tija kubwa. Aidha, amewashauri wananchi kutengeneza na kutumia teknolojia ya “greenhouse” katika maeneo yao ili iweze kuwasaidia katika kujipatia mahitaji ya mbogamboga na matunda. Amesema kuwa kufanya hivyo kutawahakikishia uhakika wa mbogamboga na matunda kwa familia na kuuza kwa watu wengine na kujiongezea kipato.
Wakati huohuo, Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya ya Mufindi, Nuhu Mwasumilwe katika ukaguzi wa mabanda amepongeza jitihada za hospitali ya rufaa ya Mbeya kununua mashine ya kusafisha figo. Amesema kuwa ununzi wa mashine hiyo utasaidia wananchi wengi wanaosumbuliwa na tatizo la figo. Amesema kuwa mashine hiyo itasaidia kupunguza muda wa wananchi kutumia kufuata huduma hiyo na badala yake kujihusisha na shughuli za kilimo.
Nuhu Mwasumilwe
Mwasumilwe ambaye pia ni Katibu Tawala Msaidizi, Sehemu ya Mipango na Uratibu katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa amepongeza ufugaji wa nyuki katika Wilaya ya Mufindi ambapo mfugaji Bahati Mhapa amekuwa akifuga nyuki kwa tija. Amesema kuwa mfugaji huyo mwenye mizinga zaidi ya 800  amekuwa akizalisha zaidi ya tani 2.5 za asali kwa mwaka. Amesema kuwa changamoto kubwa ni uhitaji wa soko la nje ambalo ni kubwa sana kuliko uwezo wa kuzalisha asali hapa nchini. Mwasumilwe ametoa wito kwa wananchi kuwekeza katika ufugaji wa nyuki kwa kiwango kikubwa ili kunufaika na soko la nje.
Akiongelea udanganyifu wa kuuza mbegu, Mwasumilwe amekemea tabia ya udanganyifu kwa baadhi ya wafanyabiashara wanaouza mbegu feki. Amesema kuwa ni vizuri wauzaji wa mbegu wakatambuliwa ili kukabiliana na wauzaji feki wa mbegu nchini.
Akiwasilisha tathmini yake alipotembelea mabanda mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya ya Kilolo, Grace Macha ametoa rai kwa wananchi kutumia teknolojia ya kufua umeme inayotengenezwa na chuo cha ufundi stadi VETA. Amesema kwa kutumia teknolojia hiyo rahisi kutasaidia kaya masikini kuwa na nishati ya umeme kwa gharama nafuu.    
Grace Macha
 Macha ambae pia ni Afisa Kilimo Mkuu katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa amewataka wananchi hasa wakulima kutumia taarifa zinazotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa nchini katika shughuli za kilimo. Amesema kuwa zipo taarifa nyingi muhimu zinazotolewa na Mamlaka hiyo zinazoweza kuwasaidia wakulima lakini haziwafikii wakulima kutokana na kutokuwa na utaratibu muafaka wa kuziunganisha taarifa hizo na wakulima.
=30=

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Habari zinazoendelea hivi sasa

SERIKALI KUWEZESHA VIJANA KUKOPA

Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa Serikali itaendelea kuwawezesha vijana kwa kuwatengenezea mazingira mazuri ya mikopo ili waweze k...