Jumamosi, 21 Februari 2015

SHULE ZA SEKONDARI ZA KATA ZAPEWA CHANGAMOTO



Na. Namsembeli Mduma, Habari Leo
Wanafunzi wa shule za serikali za kata zinazobezwa kwa kuitwa yeboyebo wametakiwa kuendelea kufanya vizuri waitoe kimasomaso serikali isikashifiwe kwa jitihada zake za kuendeleza shule hizo.
Akizungumza kwenye Ikulu ndogo mjini hapa juzi, waziri Mkuu, mizengo panda ambaye yuko kwenye ziara ya kikazi mkoani humu, alisema kilichofanywa na wanafunzi wa shule ya sekondari Igowole ya Mufindi ni ishara kuwa shule hizo zinaweza kuwa vinara wa ufaulu, tofauti na inavyofikiriwa.
Kwa mujibu wa panda, kumekuwa na mitazamo hasi miongoni mwa baadhi ya watu kuhusu shule za serikali za kata, kiasi cha kuwafanya wanaosoma katika shule hizo kukata tama wakiamini kuwa hawawezi kufaulu wakisoma kwenye shule hizo.
Hata hivyo rekodi ya matokeo ya mtihani wa kidato cha sita mwaka 2013, kama ilivyotolewa kwa waziri mkuu na mkuu wa mkoa huo, Amina Masenza zinaonesha kuwa mkoa ulifanya vizuri katika mtihani huo, ambapo asilimia 99 ya watahiniwa wote walifaulu.
Kutokana na rekodi hizo, shule ya sekondari Igowole ambayo ni ya serikali ya Kata iliongoza kitaifa, huku shule nyingine ya sekondari iitwayo Kawawa ambayo pia ipo katika wilaya ya Mufindi ilikuwa katika 10 bora kitaifa.
“ninawapongeza viongozi, walimu na wanafunzi kwa bidii mnayoionesha. Mnaitwa yeboyebo kuonesha kuwa hamuwezi, lakini cha kufurahisha ni kwamba, pamoja na changamoto nyingi mnaweza tena zaidi ya wanaomini kuwa ndio wenyewe katika masuala haya ya elimu,” alisema na kuwaomba waendeleze bidii hiyo ili serikali itoke kimasomaso.
Wakati huohuo, Masenza alimweleza waziri mkuu kuwa ufaulu wa wanafunzi wa kidato cha nne umeongezeka kutoka asilimia 52.1 mwaka 2010 hadi asilimia 65.2 mwaka 2013, jambo linalofanya mkoa huo uzidi kupata moyo wa kutukumia mbinu bora zaidi za ufundishaji kupanua uelewa.
Alitaja mafanikio mengine katika eneo la elimu kuwa ni pamoja na kufaulu kwa wanafunzi 14,650 wa darasa la saba mwaka jana, ambao ni kati ya wanafunzi 21,363, sawa na asilimia 68.5
“mwaka 2010 wanafunzi 24,035 walifanya mtihani wa darasa la saba ambapo 15,512 sawa na asilimia 64.5 walifaulu vizuri,” Masenza alisema.
Waziri Mkuu alisema, serikali inatambua changamoto zilizopo katika sekta ya Elimu na kuzitafutia ufumbuzi wa kina.  
=30=

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Habari zinazoendelea hivi sasa

SERIKALI KUWEZESHA VIJANA KUKOPA

Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa Serikali itaendelea kuwawezesha vijana kwa kuwatengenezea mazingira mazuri ya mikopo ili waweze k...