Jumapili, 22 Februari 2015

WAZIRI PINDA APONGEZA WA MAABARA YA SEKONDARI KIHESA



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Waziri Mkuu amepongeza ujenzi wa Maabara katika shule ya sekondari ya Kihesa kuwa imedhihirisha thamani halisi ya fedha.
Kauli hiyo imetolewa na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Mizengo Pinda alipokagua maendeleo ya ujenzi wa Maabara katika shule hiyo.
“Kihesa sekondari Maabara imejengwa haikukarabatiwa” alisema Mhe. Pinda. Kauli hiyo imekuja kufuatia baadhi ya maeneo kukarabati Maabara za zamani badala ya kujenga Maabara mpya. Amesema kuwa agizo la Mhe. Rais lilikuwa ni kujenga Maabara si kukarabati zilizopo. Aidha, ameoneshwa kusikitishwa na baadhi ya maeneo kubadilisha vyumba vya Madarasa kuwa Maabara. Amesema utaratibu huo unaondoa dhana ya ujenzi wa Maabara kwa sababu vyumba hivyo ni vidogo ikilinganishwa na vipimo halisi vya ramani ya sasa ya Maabara. Amesema kuwa mabadiliko hayo ya vyumba vya Madarasa kuwa Maabara kutasababisha upungufu wa vyumba vya Madarasa.
Akiongelea suala la nidhamu kwa wanafunzi, Waziri Mkuu amewapongeza walimu na wazazi kwa kusimamia nidhamu ya wanafunzi katika shule hiyo. Pongezi hizo zimetokana na tathmini ya haraka iliyofanywa na Mhe. Pinda katika shule hiyo juu ya mavazi ya wanafunzi. Amesema kuwa nidhamu inahusisha mavazi pia. Amesema sehemu nyingine alizotembelea amewakuta wanafunzi wavulana wamevaa suruali katikati ya makalio.
Wakati huohuo, mke wa Waziri Mkuu mama Tunu Pinda amechukua fursa hiyo kuwatakia heri wanafunzi wa shule ya sekondari kihesa. Amewataka wanafunzi hao kuwa ‘wasongolist’ akimaanisha kuwa wawe wanaopenda kujisomea zaidi ya mambo mengine ili kuongeza ufaulu wao. Amewataka kuendeleza nidhamu katika mavazi ili waendelee kuheshimika katika jamii inayowazunguka.
Waziri Mkuu yupo katika ziara ya kukagua shughuli mbalimbali za maendeleo katika Mkoa wa Iringa akiwa katika siku yake ya tano amefanya ziara katika Manispaa ya Iringa kwa kukagua maendeleo ya ujenzi wa Maabara pamoja na mambo mengine.
=30=

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Habari zinazoendelea hivi sasa

SERIKALI KUWEZESHA VIJANA KUKOPA

Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa Serikali itaendelea kuwawezesha vijana kwa kuwatengenezea mazingira mazuri ya mikopo ili waweze k...