Jumapili, 1 Machi 2015

PINDA APONGEZA UJENZI WA VITUO VYA AFYA IRINGA



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Waziri Mkuu Mhe. Mizengo Pinda amewapongeza wananchi wa Wilaya ya Iringa kwa kazi nzuri ya ujenzi wa Vituo vya Afya kwa lengo la kuboresha afya za wananchi wa Wilaya hiyo.
Kauli hiyo ameitoka Wilayani Mufindi alipokuwa akifanya majumuisho ya ziara yake kwa kila Wilaya.
Mhe. Pinda amesema “naomba nitumie fursa hii kuwapongeza wananchi wa Wilaya ya Iringa kwa kazi nzuri mnayoifanya katika ujenzi wa Vituo vya Afya”. Ametolea mfano Kituo cha Afya cha Mlowa alichokitembelea na kukifungua rasmi kuwa kitawapunguzia wananchi kero ya usafiri wa kwenda umbali mrefu kupata huduma ya afya. “Ni rai yangu kuwa kituo hiki kitatumika na kutoa huduma kwa wananchi wa Mlowa na majirani. Hakikisheni kituo hiki kinadumu” alisisitiza Waziri Mkuu.
Mhe. Pinda hakusita kukipongeza kituo hicho kwa kutenga dirisha maalum la kuhudumia wazee. “Nilipokuwa katika Kituo cha Afya cha Mlowa nilifarijika kuona dirisha maalum la kuhudumia wazee wenye umri mkubwa kuanzia miaka 60.” alisema Mhe. Pinda.
Ametumia nafasi hiyo kuwaasa viongozi wa Mkoa na Wilaya kuendeleza utamaduni na sera hiyo nzuri ya kuwajali wazee. Amesema kuwa kutokana na wazee kuwa wanakabiliwa na magonjwa ya kipekee yanayoendana na umri wao. Ameyataja magonjwa yanayowakabili wanaume kuwa tatizo la shinikizo la damu na saratani ya tezi dume lakini tatizo likijulikana mapema linatibika. Aidha, ameyataja magonjwa yanayowakabili wanawake zaidi kuwa ni saratani ya mlango wa kizazi, UTI, Fistula na Malaria. Wananchi wakielimishwa dalili za magonjwa hayo watakwenda Kituo cha Afya mapema na hivyo kupunguza uwezekano wa kuugua kwa muda mrefu na pengine kupoteza maisha. Amewataka viongozi kuwahamasisha wananchi kujenga tabia ya kupima afya mapema ili kujua kuwepo kwa maradhi.
Waziri Mkuu, akiongelea skimu ya umwagiliaji ya Magozi, amesema kuwa changamoto kubwa aliyoiona inayowakumba wananchi na vikundi vya wakulima wa mpunga wa vijiji vya Mkombilenga, Ilolompya na Magozi ni njia bora ya kutumia kwa tija zana bora za kilimo zilizopo kwa lengo la kuongeza uzalishaji. Katika skimu hiyo Waziri Mkuu alimshauri Mkuu wa Mkoa kuwasiliana na Mkoa wa Morogoro ili kujifunza namna kampuni ya mpunga ya Kilombero inavyoshirikisha wakulima wadogo katika kilimo cha mpunga.
Aidha, aliwashauri kuungana na kutengeneza vijishamba vyao katika mashamba makubwa ya pamoja ili opereresheni za kilimo zifanyike kwa pamoja.
=30=

   

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Habari zinazoendelea hivi sasa

SERIKALI KUWEZESHA VIJANA KUKOPA

Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa Serikali itaendelea kuwawezesha vijana kwa kuwatengenezea mazingira mazuri ya mikopo ili waweze k...