Ijumaa, 15 Mei 2015

IRINGA KINARA ELIMU YA MSINGI KWA MIAKA 15 MFULULIZO



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Mkoa wa Iringa umeendelea kufanya vizuri katika ufaulu wa mitihani ya elimu ya msingi kwa zaidi ya miaka 15 mfululizo.

Kauli hiyo imetolewa na Afisa Michezo Mkoa wa Iringa, Bw. Kenneth Komba alipowasilisha taarifa ya sekta ya elimu kwa niaba ya Afisa Elimu Mkoa wa Iringa katika kikao baina ya viongozi wa Mkoa na viongozi wa dini kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa ofisi ya mkuu wa mkoa wa Iringa.

Bw. Komba amesema “mkoa umeendelea kushika nafasi ya tatu na nne kitaifa katika ufaulu kwenye mtihani wa kuhitimu elimu ya msingi kwa kipindi cha miaka 16 mfululizo”. Amesema kuwa mwaka 2014 shule za kwanza na kumi kitaifa katika mtihani wa kidato cha sita zilitoka katika mkoa wa Iringa. Amezitaja shule hizo za sekondari kuwa ni Igowole iliyoshika nafasi ya kwanza na Kawawa iliyoshika nafasi ya 10.

Akiongelea uandikishaji wanafunzi wa madarasa ya awali na msingi, Afisa Michezo amesema kuwa uandikishaji huo unaendelea kwa zaidi ya asilimia 99 kwa kila halmashauri za mkoa wa Iringa. 

Akiongelea changamoto zinazoikabili sekta ya elimu mkoani Iringa, Bw. Komba ameitaja changamoto kubwa kuwa ni upungufu wa walimu wa masomo ya sayansi kwa shule za sekondari. Changamoto nyingine ameitaja kuwa ni madeni makubwa ya chakula kwa shule za bweni.

Mkoa wa Iringa una jumla ya shule za msingi 487 na shule 160 zikiwa ni za sekondari.
=30= 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Habari zinazoendelea hivi sasa

SERIKALI KUWEZESHA VIJANA KUKOPA

Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa Serikali itaendelea kuwawezesha vijana kwa kuwatengenezea mazingira mazuri ya mikopo ili waweze k...