Alhamisi, 30 Julai 2015

IRUWASA WATAKIWA KUTOA HUDUMA BORA KWA WATEJA



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Mamlaka ya majisafi na usafi wa mazingira Iringa (IRUWASA) wametakiwa kutoa huduma bora, kwa wakati na bei halali ili kuondoa malalamiko ya wateja.

Kauli hiyo ilitolewa na mkuu wa mkoa wa Iringa, Amina Masenza alipokuwa akifungua taftishi juu ya maombi ya kurekebisha bei za huduma ya majisafi na majitaka yaliyotolewa na IRUWASA katika ukumbi wa Veta mjini Iringa.

Masenza alisema kuwa watumiaji wa huduma ya maji wanayo haki ya kupata huduma kwa wakati, kwa bei halali, kuhoji ubora wa huduma wanayopata na kutoa malalamiko kwa watoa huduma, na ikibidi kwa EWURA ili kero zote ziondolewe. Alisema pamoja na haki hiyo, watumiaji wa huduma wanao wajibu, kwa sababu “haki bila wajibu ni vurugu, na wajibu bila haki ni utumwa”. 

Alisema “watumiaji wa huduma za maji na uondoshaji wa majitaka wana wajibu wa kulipia huduma hizo kikamilifu na kwa wakati muafaka. Aidha, wanao wajibu wa kuithamini na kuihifadhi miundombinu iliyopo kwa manufaa yao, watoa huduma na Taifa kwa ujumla”.

Kwa upande wa watoa huduma, mkuu wa mkoa alisema kuwa kwa mujibu wa sheria, watoa huduma wanaodhibitiwa na EWURA kama IRUWASA, wana wajibu wa kutoa taarifa sahihi za utendaji wao kwa wateja wao na kwa EWURA. Alisema jukumu lao la msingi ni kutoa huduma na bidhaa bora na kwa wakati kwa watumiaji wengi zaidi. Aliongeza kuwa watoa huduma wana haki zao za msingi ikiwa ni pamoja na kupata marejesho ya mitaji yao na faida ili waweze kuwekeza zaidi katika miundombinu na mambo mengine ili huduma kama za majisafi na uondoshaji wa majitaka ziweze kuwafikia watu wengi zaidi.

Akiongelea matarajio ya serikali, alisema “serikali inatarajia utendaji mahiri wa EWURA utakuwa chachu ya kuboresha utoaji wa huduma za majisafi na uondoshaji wa majitaka hapa nchini. Uwekezaji katika sekta hii utaongeza upatikanaji na ubora wa huduma hii na hivyo kuleta ufanisi endelevu na wenye kuzingatia uboreshaji wa mazingira kwa faida yetu na ya vizazi vijavyo” alisisitiza Masenza. 

Alisema “taftishi hii ya leo ni miongoni mwa juhudi za EWURA katika kushirikisha wadau na kupata maoni yao kuhusu huduma zinazotolewa na IRUWASA na mipango itakayowasilishwa mbele yenu katika sekta hii muhimu ya huduma za majisafi na uondoshaji wa majitaka. Sisi ndio watumiaji wa huduma hizo na sisi ndio wenye maoni kuhusiana na ubora wa huduma tunazozipata na changamoto mbalimbali zinazoendana na upatikanaji wa huduma hizo”.
=30=

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Habari zinazoendelea hivi sasa

SERIKALI KUWEZESHA VIJANA KUKOPA

Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa Serikali itaendelea kuwawezesha vijana kwa kuwatengenezea mazingira mazuri ya mikopo ili waweze k...