Alhamisi, 30 Julai 2015

WATUMISHI RS WATAKIWA KUTOA TAARIFA ZA UKIUKWAJI WA MAADILI



Na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Watumishi wa ofisi ya mkuu wa mkoa wa Iringa wametakiwa kutoa taarifa zinazohusu ukiukwaji wa maadili na uadilifu ili haki iweze kutendeka.

Kauli hiyo ilitolewa na mwenyekiti wa Kamati ya kudhibiti uadilifu katika ofisi ya mkuu wa mkoa wa Iringa, Kilasi Mwakilasi alipokuwa akifafanua uwepo na utendaji kazi wa kamati yake.

Mwakilasi ambaye pia ni Katibu Tawala Msaidizi, Sehemu ya Miundombinu alisema kuwa kamati ya kudhibiti uadilifu ni chombo kilichoundwa kwa mujibu wa taratibu zilizowekwa na serikali kwa ajili ya kuangalia maandili kikiwa na lengo la kusimamia na kudhibiti utendaji wa kimaadili kwa watumishi wa nyanja zote katika ofisi ya mkuu wa mkoa wa Iringa.

Alisema kuwa kamati hiyo inaangalia kwa kiasi gani maadili yanafuatwa katika kuwahudumia wananchi na baina ya watumishi wenyewe. Alisema kuwa chombo hicho bado hakifahamiki kwa watumishi wote pamoja na kuwa na jukumu muhimu la kudhibiti katika utumishi ofisini hapo.

Mwalikasi alisema kuwa katika ofisi ya mkuu wa mkoa, kamati hiyo inaangalia kuanzia kwa viongozi waandamizi kama wakuu wa sehemu na vitengo wanatenda kazi kwa kufuata maadili pasipo kuwanyanyasa wala kuwaonea watumishi walio chini yao. Pamoja na mambo mengine masuala ya rushwa yanaangaliwa kwa uzito mkubwa. Aliyataja mambo mengine kuwa ni unyanyasaji wa aina zote, uadilifu katika utoaji wa huduma kwa wateja wa nje, matumizi ya lugha yenye staha na mavazi.

Akiongelea hali ya maadili na uadilifu katika ofisi ya mkuu wa mkoa, Mwenyekiti wa kamati ya kusimamia maadili alisema  kuwa hali ya maadili na uadilifu ni ya kuridhisha. Alisema kuwa kamati yake inajiridhisha kutokana na kutokuwapo kwa malalamiko kutoka kwa watumishi na wapokea huduma wa nje. Kwa upande wa changamoto, alisema kuwa kamati yake inakabiliwa na changamoto ya kufahamika kwa watumishi pamoja na rasilimali bajeti. Aidha, aliwataka watumishi wote pindi wanapokuwa na tatizo la kimaadili na uadilifu kuliwasilisha katika kamati yake ili haki iweze kuchukua mkondo wake.

Kamati ya kudhibiti maadili iliundwa na wajumbe wanne kutoka sehemu ya miundombinu, utawala, elimu na afya waliochaguliwa kutokana na kuwa na maadili mema katika jamii.
=30=

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Habari zinazoendelea hivi sasa

SERIKALI KUWEZESHA VIJANA KUKOPA

Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa Serikali itaendelea kuwawezesha vijana kwa kuwatengenezea mazingira mazuri ya mikopo ili waweze k...