Alhamisi, 30 Julai 2015

RAS WAMOJA APONGEZA UTENDAJI WA WATUMISHI MKOANI



Watumishi wa ofisi ya mkuu wa mkoa wa Iringa wamepongezwa kwa utendaji kazi pamoja na changamoto ya ufinyu wa bajeti.

Pongezi hizo zilitolewa na Katibu Tawala Mkoa wa Iringa, Wamoja Ayubu alipokuwa akiongea na watumishi wote wa ofisi ya mkuu wa mkoa hivi karibuni katika ukumbi wa mikutano wa ofisi ya mkuu wa mkoa.
Katibu Tawala Mkoa wa Iringa Wamoja Ayubu (kushoto) akifafanua jambo

Wamoja alisema “nianze kwa kuwapongeza watumishi wote kwa nafasi zenu kwa utendaji kazi katika ofisi hii. Mafanikio ya mkoa yanatokana na utendaji wenu mzuri wa kazi. Ni matumaini yangu mtaongeza juhudi zaidi katika mwaka huu wa fedha 2015/2016 pamoja na changamoto ya bajeti na rasilimali tuliyonayo”.

Amewataka watumishi wote kufanya kazi kwa kujaliana na kusisitiza kuwa kidogo kitakachopatikana kigawanywe kwa usawa na haki ili wote waweze kuwahudumia wananchi vizuri. Amesema kuwa kwa kuwa muda mwingi watumishi wanautumia katika maeneo yao ya kazi, wao ni familia moja hivyo suala la upendo ni  muhimu sana. “Muda mwingi tunatumia ofisini hivyo sisi ni ndugu. Mtu akiwa na shida hata kama huna uwezo wa kumtatulia hebu mshauri. Lazima tuone namna gani tutapunguziana msongo wa mawazo” alisisitiza Wamoja.

Akiongelea kufanya kazi kwa uwazi, Katibu Tawala Mkoa wa Iringa aliwataka wakuu wa sehemu na vitengo katika ofisi ya mkuu wa mkoa kufanya kazi kwa uwazi na kuwashirikisha watumishi walio chini yao. Amesema “ushirikishaji ni jambo zuri katika kuondoa manung’uniko ya watumishi. Cha msingi ni kupeana taarifa katika sehemu na vitengo vyenu ili kuondokana na taarifa za upotoshaji zinazoweza kujitokeza”. 

Wakati huohuo Katibu Tawala Msaidizi, Sehemu ya Utawala na Rasilimali watu Scolastica Mlawi alitumia kikao hicho kuwakumbusha watumishi kuzingatia sheria na kanuni za utumishi wa umma katika kipindi chote cha utumishi wao. Aidha, aliwakumbusha watumishi kuwa wanawajibu wa kuwahi kazini na kutekeleza majukumu yao kwa mujibu wa muundo wa utumishi. Alisema kuwa kila mtumishi anawajibu wa kusaini kitabu cha mahudhurio kwa mujibu wa taratibu za ofisi. 

Akiongelea mavazi, aliwataka watumishi kuvaa vizuri kama waraka wa mavazi unavyoelekeza.
Kikao baina ya Katibu Tawala Mkoa na watumishi ni muendelezo wa vikao vya kujadili changamoto na mafanikio katika ofisi ya mkuu wa mkoa na kufahamishana hali halisi ya ofisi inavyokwenda kwa kipindi husika.
=30=

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Habari zinazoendelea hivi sasa

SERIKALI KUWEZESHA VIJANA KUKOPA

Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa Serikali itaendelea kuwawezesha vijana kwa kuwatengenezea mazingira mazuri ya mikopo ili waweze k...