Alhamisi, 30 Julai 2015

KUU IRINGA YATATUA MGOGORO WA WACHIMBAJI DHAHABU NA MUWEKEZAJI


Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa - IRINGA

Serikari mkoani Iringa imemaliza mgogoro baina ya muwekezaja na wachimbaji wadogo katika machimbo ya dhahabu katika kijiji cha Ulata.


Akitoa taarifa kwa waandishi wa habari ofisini kwake, mkuu wa mkoa wa Iringa Amina Masenza amesema kuwa mgogoro huo ulikuwa baina ya muwekezaji katika machimbo hayo ya dhahabu Ibrahim Msigwa, wachimbaji wadogo na kijiji cha Ulata.

Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama Mkoa wa Iringa Amina Masenza

Mkuu wa mkoa wa Iringa ambaye pia ni mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama mkoa alilazimika kutembelea eneo la mgogoro akiambatana na kamati yake ya ulinzi na usalama kuona hali halisi ya eneo husika kufuatia vifo vya wachimbaji watano waliofukiwa katika moja ya miduara katika machimbo hayo hivi karibuni.


Masenza aliyataja makubaliano yaliyofikiwa baina ya muwekezaji, uongozi wa kijiji, wachimbaji wadogo na kamati ya ulinzi na usalama mkoa kuwa ni muwekezaji katika machimbo hayo Ibrahim Msigwa mwenye leseni sita za uchimbaji atoe hisa mbili kwa kila leseni na kukipatia kijiji cha Ulata. Hisa hizo zilielekezwa kuwa zitatumika katika shughuli za maendeleo za kijiji hicho. Makubaliano mengine yaliyofikiwa ni mwenyekiti wa kijiji cha Ulata alitakiwa kuvaa vazi la uongozi na kuwaongoza wanakijiji kwa mujibu wa taratibu na miiko ya uongozi ili kuhakikisha usalama unakuwepo katika kijiji hicho. Pia ofisi ya madini kanda ya kusini magharibi ikakague usalama wa eneo lote la machimbo. 

Aidha, mwenyekiti alitakiwa kuitisha kikao cha kijiji na kufafanua makubaliano hayo ili kijiji kiingie katika umiliki wa machimbo hayo kihalali.


Wakati huohuo, mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama mkoa wa Iringa aliitaka ofisi ya kanda ya madini kuwajengea uwezo wachimbaji vijana ili wakopesheke waweze kuchimba kwa mujibu wa taratibu na ufanisi. Aidha, amewataka wachimbaji vijana kuachana na tabia ya anasa ikiwa ni pamoja na matumizi yaliyokithiri ya vilevi na kujilinda na maambukizi ya virusi vya ukimwi katika eneo la machimbo. “Viroba vinawaua wanangu na kuharibu mapafu. Mkishalewa hamuwezi kufanya maamuzi sahihi ikiwa ni pamoja na kukumbuka kuwa kuna Ukimwi” alisisitiza Masenza.


Aliwakumbusha wachimbaji hao kuwa hakuna mtu au kikundi cha watu kilicho juu ya sheria  na kuwataka kufuata sheria na taratibu za nchi. Amekemea tabia za kuwapiga na kuwafanyia vurugu maafisa wa serikali na raia wanapokuwa wakitekeleza majukumu yao. “Nchi hii ni huru na ni yetu sote, hakuna aliye juu ya sheria na haki ya kupiga wengine na kuwafanyia vurugu. Tabia hiyo ni marufuku katika mkoa ninaouongoza mimi” alisisitiza Masenza.


Nae Mhandisi Migodi, kanda ya kusini magharibi Zephania Msungi alisema awali hali ilikuwa tete katika machimbo hayo kwa sababu maafisa kutoka ofisi ya madini ya kanda hawakuruhusiwa kuingia katika eneo hilo. Alisema kwa muafaka huo itakuwa rahisi kutekeleza jukumu lao la kusimamia sheria ya madini ya mwaka 2010 na kanuni zake ikiwa ni pamoja na kuhakikisha serikali inapata mapato yake kutokana na shughuli za machimbo.


Akiongelea hali ya usalama katika machimbo hayo ya dhahabu, Mhandisi Mgungi alisema kuwa hali ya usalama siyo ya kuridhisha kwa sasa. Ofisi yake itaenda kukagua eneo hilo na kushauri juu ya uchimbaji salama kwa usalama wa wachimbaji wenyewe.

=30=

 




Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Habari zinazoendelea hivi sasa

SERIKALI KUWEZESHA VIJANA KUKOPA

Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa Serikali itaendelea kuwawezesha vijana kwa kuwatengenezea mazingira mazuri ya mikopo ili waweze k...