Ijumaa, 1 Julai 2016

KILOLO YAPUNGUZA MALARIA KWA 11%



Na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Halmashauri ya Wilaya ya Kilolo imepunguza kiwango cha ugonjwa wa Malaria hadi kufikia asilimia 11.3 mwaka 2016.

Kauli hiyo hiyo ilitolewa na Katibu Tawala Wilaya ya Kilolo, Yusuph Msawanga wakati akisoma risala ya utii ya wananchi wa Wilaya ya Kilolo katika uwanja wa soko wakati Mwenge wa Uhuru ukiwa wilayani hapa.

Msawanga alisema kuwa ugonjwa wa Malaria ni miongoni mwa magonjwa yanayoongoza kwa kuathiri watu wengi wilayani Kilolo.

Kwa kipindi cha mwaka 2016 kati ya wagonjwa 170,168 waliofika jengo la wagonjwa wa nje 19,303 walipimwa na kugundulika kuwa na vimelea vya Malaria, hii ni sawa asilimia 11.3 ya wagonjwa wote waliofika jengo la wagonjwa wa nje. Takwimu hizi zinabainisha kuwa kiwango cha ugonjwa wa Malaria kilipungua kutoka asilimia 23.6 mwaka 2015 na kufikia asilimia 11.3 mwaka 2016” alisema Msawanga.

Aliongeza kuwa jumla ya wagonjwa 3,732 waliokuwa wamelazwa, kati yao 537 waligundulika kuwa na malaria baada ya kupimwa sawa na asilimia 14.4 ya wagonjwa wote waliolazwa. Alisema kuwa kiwango cha ugonjwa wa malaria kimepungua kwa asilimia 6.5 toka asilimia 20.9 ya mwaka 2014 hadi 14.4 mwaka 2016.

Katibu Tawala huyo katika kuhakikisha ugonjwa wa Malaria unakuwa historia, wilaya ya Kilolo inaendelea kuielimisha jamii juu ya matumizi ya sahihi ya vyandarua, kupima na kutoa tiba sahihi kwa wagonjwa wa Malaria.

Juhudi nyingine alizitaja kuwa ni kuihamasisha jamii kupima mapema mara wanapohisi kuumwa. Nyingine ni utoaji wa dawa za tiba kinga kabla ya madhara kwa kutumia dawa ya mseto kwa mama wajawazito na kuhamasisha jamii juu ya usafi wa mazingira ili kuondoa uwezekano wa mazalia ya mbu waenezao Malaria.
=30=

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Habari zinazoendelea hivi sasa

SERIKALI KUWEZESHA VIJANA KUKOPA

Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa Serikali itaendelea kuwawezesha vijana kwa kuwatengenezea mazingira mazuri ya mikopo ili waweze k...