Ijumaa, 1 Julai 2016

MANISPAA YAPIMA VVU WAJAWAZITO 6,853



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Manispaa ya Iringa imefanikiwa kupima wanawake wajawazito 6,853 waliohudhuria kliniki katika kutekeleza mkakati wa Mkoa wa kupambana na Ukimwi wenye lengo la kupunguza kiwango cha maambukizi hadi asilimia saba.

Taarifa hiyo ilitolewa na Afisa Tawala katika Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Iringa, Olgatho Mwinuka alisema kuwa Manispaa ya Iringa katika kuendeleza mapambano dhidi ya Ukimwi chini ya kaulimbiu isemayo “tanzania bila maambukizi mapya, unyanyapaa na vifo vitokanavyo na ukimwi inawezekana” Manispaa kwa kushirikiana na wadau inatekeleza mkaakti wa Mkoa wa kupambana na Ukimwi, wenye lengo la kupunguza kiwango cha maambukizi toka asilimia 9.1 hadi asilimia 7 ifikapo mwaka 2017,

katika utoaji wa huduma ya kuzuia maambukizi toka kwa mama kwenda kwa mtoto. Alisema kuwa jumla ya wajawazito 6,853 walihudhuria kliniki ya afya ya uzazi kwa kipindi cha Januari hadi Mei, 2016, kati yao 2,262 walipimwa maambukizi ya VVU, 122 sawa na asilimia 5.4 walikutwa na maambukizi. Aidha, vituo vinavyotoa huduma hiyo vimeongezeka toka 18 mwaka 2015 hadi 19 mwaka 2016.

Aliongeza kuwa Manispaa kwa kushirikiana na wadau wake imeendelea kutoa elimu ya kujikinga na maradhi ya Ukimwi kwa makundi yote. Kampeni ya tohara kwa wanaume inaendelea, ambapo jumla ya wanaume 1,449 walitahiriwa kwa mwaka 2015. Vilevile, hamasa juu ya upimaji na utoaji wa ushauri nasaha inaendelea kutolewa, ambapo watu 18,011 (8,167 me, 9,844 ke), kati yao 1,628 (634 me, 994 ke) sawa na 9% walikutwa na maambukizi ya VVU kwa mwaka 2015.

Aidha, vituo vya ushauri nasaha na upimaji vimeongezeka toka vituo 14 mwaka 2010 hadi vituo 18 mwaka 2016. Haki za watu wanaoishi na VVU/UKIMWI zimeendelea kutetewa kwa lengo la kuondoa unyanyapaa na ubaguzi katika jamii.

Wakati huohuo, afisa tawala huyo alisema kuwa mapambano dhidi ya ugonjwa wa malaria, kupitia ujumbe usemao “wekeza katika maisha ya baadaye” chini ya kauli mbiu isemayo “tokomeza malaria” Manispaa inaendelea kutoa elimu kuhusu namna malaria inavyoenezwa, jinsi ya kujikinga, upimaji wa afya na matumizi ya dawa. Aliongeza kuwa elimu hiyo imepelekea kupungua kwa ugonjwa wa malaria kwa watoto chini ya umri wa miaka mitano, kutoka wagonjwa 30,795 mwaka 2012 hadi wagonjwa 4,620 mwaka 2015.

Vilevile, matumizi ya vyandarua yameendelea kuhimizwa na katika kipindi cha mwezi Januari mpaka Machi 2016, jumla ya vyandarua 113,418 vimegawiwa kwenye kaya 43,682 katika Manispaa ya Iringa.

Mwenge wa Uhuru katika Manispaa ya Iringa ulikimbizwa umbali wa kilomita 64.4 katika kata saba, jumla ya miradi sita yenye thamani ya shilingi bilioni 7,139,993,299 imefikiwa, kati ya miradi hiyo mitatu ni ya huduma za kijamii, mmoja ni wa elimu, mmoja ni wa uzalishaji kupitia kilimo cha umwagiliaji na mwingine ni wa kuhifadhi na kutunza mazingira.
=30=

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Habari zinazoendelea hivi sasa

SERIKALI KUWEZESHA VIJANA KUKOPA

Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa Serikali itaendelea kuwawezesha vijana kwa kuwatengenezea mazingira mazuri ya mikopo ili waweze k...