Jumanne, 27 Juni 2017

JAMII YATAKIWA KUTOA TAARIFA ZA RUSHWA TAKUKURU



Na. Mwandishi Maalum, Kilolo

Jamii imetakiwa kutoa taarifa za vitendo vya rushwa na viashiria vyake kwa Taasisi ya kuzuia na kupambana na rushwa nchini (Takukuru) ili kuwa na taifa lisilokuwa na rushwa.

Wito huo ulitolewa na Mkuu wa Takukuru wilaya ya Kilolo, Fuja Ngalo alipowasilisha mada juu ya umuhimu wa watumishi wa umma kupinga vitendo vya rushwa mahala pa kazi katika wiki ya Utumishi wa Umma iliyoandaliwa na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa na kufanyika katika Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Kilolo wiki iliyopita.

Ngalo alisema “tunahitaji ushirikiano wa watumishi na wananchi kwa ujumla kwa sababu sisi kama Taasisi ya kuzuia na kupambana na rushwa peke yetu hatuwezi”. Alisema kuwa vitendo vya rushwa vinafanyika katika jamii, hivyo, jamii ina wajibu wa kutoa taarifa za vitendo vya rushwa na viashiria vyake ili viweze kufanyiwa kazi kwa mujibu wa sheria za nchi. “Sheria ya kuzuia na kupambana na rushwa namba 11 ya mwaka 2007 kifungu cha 39, kinaelezea wajibu wa mwananchi katika kuzuia na kupambana na rushwa nchini” alisema Ngalo. 

Alisema kuwa katika kutengeneza mazingira rafiki baina ya taasisi hiyo na jamii, imezindua programu ijulikanayo kama longa nasi kwa namba 113 ambayo mteja atapiga na kuongea moja kwa moja na Takukuru na kutoa taarifa za vitendo vya rushwa bila malipo.

Nae, Afisa Uelimishaji wa Takukuru wilaya ya Kilolo, Ezekiel Mwenda alisme kuwa rushwa ni matumizi mabaya ya madaraka kwa mtumishi wa umma. Alisema kuwa Takukuru wilaya ya Kilolo itawashughulikia wote watakaojihusisha na vitendo vya rushwa kwa mujibu wa sheria za nchi. 

Aliongeza kuwa wananchi wanakuwa na hofu kutoa taarifa za vitendo vya rushwa na kufifisha mapambano dhidi ya rushwa. Alisema kuwa katika kumlinda mtoa taarifa, Takukuru ina mfumo wa kinga kwa mtoa taarifa siku zote. Ulinzi wa mtoa taarifa kuhusinana na vitendo vya rushwa au ushahidi mahakamani. “Kifungu 51 (a) kinatoa kinga kutajwa kwa jina, makazi, au anuani ya aliyetoa taarifa kuhusiana na vitendo vya rushwa kwa shahidi” alisema Mwenda. Aliongeza kuwa “Takukuru hatufanyi kazi kwa kumuonea mtu bali tunafanya kazi kwa uthibitisho ili tusimuonee mtu. Tushirikiane kwenye taarifa na kutoa ushahidi ili kukomesha rushwa wilayani Kilolo” alisema Mwenda.

Katibu Tawala msaidizi, Sehemu ya Utawala na Rasilimali watu katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Lucas Kambelenje alisema kuwa mkoa uliona ni muhimu kuishirikisha Takukuru katika maadhimisho ya wiki ya Utumishi wa Umma ili waweze kutoa elimu kwa watumishi ili wawe mabalozi wazuri katika mapambano dhidi ya rushwa. 

Ni matarajio yangu kuwa baada ya mada kutoka Takukuru watumishi wote watakuwa na uelewa mkubwa juu ya vitendo vya rushwa na viashiria vyake” alisema Kambelenje.

=30=

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Habari zinazoendelea hivi sasa

SERIKALI KUWEZESHA VIJANA KUKOPA

Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa Serikali itaendelea kuwawezesha vijana kwa kuwatengenezea mazingira mazuri ya mikopo ili waweze k...