Jumanne, 27 Juni 2017

MA-DAS WATAKIWA KUFANYA VIKAO NA WATUMISHI


Na. Mwandishi Maalum Iringa
Makatibu Tawala wa Wilaya za Mkoa wa Iringa wametakiwa kufanya vikao vya kila robo mwaka na watumishi wanaowasimamia ili kutatua kero zinazowakabili.

Agizo hilo lilitolewa na Katibu Tawala msaidizi, Sehemu ya Menejimenti ya rasilimali watu katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Lucas Kambelenje alipokuwa akiongea na watumishi wa Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Iringa katika ukumbi wa mikutano wa ofisi hiyo jana.
 
Ktibu Tawala Msaidizi- Sehemu ya Utawala, Lucas Kambelenje
Kambelenje alisema kuwa watumishi katika ngazi ya wilaya wamekuwa na kero nyingi ambazo utatuzi wake upo katika ngazi ya wilaya. Alisema suluhisho la kero hizo ni Makatibu Tawala wa Wilaya kufanya vikao na watumishi wote wanaowasimamia ili kusikiliza na kuondoa kero zinazowakabili. “Watumishi wengi wanakabiliwa na kero ya kutokuelewa baadhi ya miundo na miongozo ya serikali. Na jambo hili na ufafanuzi wake ni jukumu lenu Makatibu Tawala wa Wilaya. Kufanya hivyo kutaondoa kero na manung’uniko miongoni mwa watumishi mnaowasimamia na hali ya ofisi zenu na utendaji itakuwa bora zaidi” alisema Kambelenje.

Akiongelea suala la mipango na bajeti, Kambelenje aliwataka Makatibu Tawala wa Wilaya kuwashirikisha watumishi katika mipango na bajeti ya wilaya. Alisema kuwa ushirikishaji watumishi hao kutawajengea uelewa mpana wa hali ya bajeti katika ofisi zao na kuondoa malalamiko. Alisema kuwa watumishi wanalalamika kutokana na kutofahamu hali ya bajeti katika ofisi hizo.

Wakati huohuo, Afisa Utumishi katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Olgatho Mwinuka aliwataka watumishi hao kufuata taratibu katika kuomba likizo mbalimbali ikiwemo likizo ya mwaka. “Likizo ya mwaka ni haki ya kila mtumishi. Lakini likizo hiyo inataratibu zake kama zilivyoelezwa katika Kanuni za kudumu za Utumishi wa Umma, toleo namba tatu la mwaka 2009 kifungu H”. Alisema kuwa mtumishi wa umma anatakiwa kuomba likizo yake ya mwaka ndani ya mzunguko wa likizo hiyo kwa kuandika barua ya maombi siku 14 kabla ya kuanza likizo na kuambatanisha na fomu ya maombi ya likizo husika. 

Alisema kuwa mtumishi wa umma haruhusiwi kuondoka katika kituo chake cha  kazi kabla ya kujibiwa kuwa ruhusa yake imekubaliwa kwa barua na kupatiwa nakala ya fomu ya likizo hiyo. “Mtumishi wa umma kuondoka kituoni na kuanza likizo bila kupitishwa na mwajili wake ni utoro kazini na mtumishi huyo anatakiwa kuadhibiwa kwa mujibu wa taratibu za utumishi wa umma. Ikumbukwe kuwa mwajili anaweza kusitisha likizo ya mtumishi kutokana na majukumu ya kazi yaliyopo kwa wakati huo” alisisitiza Mwinuka.
 
Afisa Utumishi Olgatho Mwinuka
Aliongeza kuwa likizo ya mwaka ya mtumishi ni siku 28 na mtumishi atalipwa nauli ya likizo kila baada ya kupita likizo moja. Aliwataja wanufaika wa malipo ya nauli ya likizo kuwa ni mtumishi mume au mke, watoto au wategemezi wanne baada ya kuwasilisha vyeti vya kuzaliwa au hati ya kiapo toka mahakamani kwa wategemezi.

Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa inaadhimisha wiki ya Utumishi wa Umma tarehe 16-23/6/2017 kwa kutembelea watumishi wa makao makuu ya mkoa, Ofisi za Wakuu wa Wilaya na hospitali ya rufaa ya Mkoa na kutoa mada mbalimbali zinazohusu haki na wajibu wa mtumishi wa umma, mapambano dhidi ya maambukizi ya virusi vya ukimwi, mapambano dhidi ya rushwa na kusikiliza na kutatua kero za watumishi.
=30=

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Habari zinazoendelea hivi sasa

SERIKALI KUWEZESHA VIJANA KUKOPA

Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa Serikali itaendelea kuwawezesha vijana kwa kuwatengenezea mazingira mazuri ya mikopo ili waweze k...