Jumanne, 27 Juni 2017

OFISI YA MKUU WA WILAYA IRINGA YATAKIWA KUJIEPUSHA NA RUSHWA



Na. Mwandishi Maalum, Iringa
Watumishi wa Umma mkoani Iringa wametakiwa kujiepusha na vitendo vya rushwa wanapowahudumia wananchi ili wananchi wanufaike na huduma wanazopatiwa.

Rai hiyo ilitolewa na Afisa Uchunguzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) Mkoa wa Iringa, Evarist Shija alipowasilsiha mada juu ya mapambano dhidi ya rushwa mahala pa kazi kwa watumishi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Iringa katika maadhimisho ya wiki ya Utumishi wa Umma yaliyoandaliwa na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa na kufanyika katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Iringa hivi karibuni.
 
Watumishi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Iringa akifuatilia mada ya Evarist Shija kutoka Takukuru Iringa
Shija alisema kuwa rushwa ni matumizi mabaya ya ofisi ya umma, mali ya umma na dhamana aliyonayo mtu kwa niaba ya umma na akaamua kuitumia kwa manufaa yake binafsi. Alisema kuwa tendo la rushwa hutokea pale mtumishi anapoamua kupindisha sheria na taratibu za nchi kwa nia ya kujipatia fedha au kitu chochote chenye thamani hata kama kitu hicho kina thamani ndogo. Alisema kuwa kutokana na hali hiyo, watumishi wa umma wanatakiwa kujiepusha na vitendo vya rushwa na viashiria vyovyote vya vitendo hivyo katika utumishi wao. “Mpokea rushwa huwa katika nafasi yenye mamlaka au nafasi ya kutoa maamuzi yatakayo muathiri anayetoa rushwa. Rushwa hutokea katika utumishi wa umma na hata katika sekta binafsi” alisisitiza Shija.

Shija alisema kuwa kwa mujibu wa sheria ya kuzuia na kupambana na rushwa namba 11 ya mwaka 2007, imeharamisha vitendo vya rushwa kuwa jinai na inayataja makosa ya rushwa bayana.

Akiongelea kanuzi za maadili, Afisa uchunguzi huyo aliyataja maadili kuwa ni sheria, taratibu na kanuni zilizokubalika katika jamii au kundi kama muongozo wa mahusiano kati yao na namna wanavyoendesha maisha yao. “Kanuni hizi zinatambulisha mambo mazuri ya kufanya dhidi ya yale mabaya yasiyostahili kufanywa na kwa kila unalotenda kuna tuzo au adhabu yake. Hivyo, kila mtumishi wa umma ana wajibu wa kufuata kanuni za maadili katika utendaji wake wa kazi” alisisitiza Shija.

Shija aliyataja maadili hayo kuwa ni uadilifu, kuwajibika kwa umma, kuheshimu sheria na matumizi sahihi ya taarifa. Aidha, alizitaja kanuni za maadili ya viongozi na watumishi wa umma kuwa ni kutoa huduma bora kwa wananchi, utii kwa serikali na wananchi wake, kuwa na bidii ya kazi na kutoa huduma bila upendeleo. Kanuni nyingine ni kufanya kazi kwa uadilifu, kuwajibika kwa umma, kuheshimu sheria na matumizi sahihi ya taarifa.

Akiongelea umuhimu wa kuzingatia maadili na kuepuka vitendo vya rushwa kwa watumishi wa umma, Shija alisema kuwa ni kuendelea kujenga imani ya wananchi juu ya uadilifu wa serikali yao na kuondoa migongano ya kimahusiano kazini. Kuhakikisha yanakuwepo matumizi mazuri ya fedha na rasilimali nyingine na kuleta tija kwa kuongeza thamani ya fedha katika miradi na huduma zinazotolewa. Vilevile, kufuata maadili ni muhimu katika kudhibiti mianya ya rushwa na ukiukwaji wa maadili, kuleta tija mahali pa kazi na kudhibiti matumizi ya madaraka waliyonayo viongozi na watumishi.

Maadhimisho ya wiki ya Utumishi wa Umma mwaka 2017 yanaongozwa na kaulimbiu isemayo ‘kuimarisha ushirikishwaji wa jamii katika utoaji huduma: vijana washirikishwe kuleta mabadiliko barani afrika’. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa inaadhimisha wiki ya Utumishi wa Umma tarehe 16-23/6/2017 kwa kutembelea watumishi wa makao makuu ya mkoa, Ofisi za Wakuu wa Wilaya na hospitali ya rufaa ya Mkoa na kutoa mada mbalimbali zinazohusu haki na wajibu wa mtumishi wa umma, mapambano dhidi ya maambukizi ya virusi vya ukimwi, mapambano dhidi ya rushwa na kusikiliza na kutatua kero za watumishi.
=30

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Habari zinazoendelea hivi sasa

SERIKALI KUWEZESHA VIJANA KUKOPA

Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa Serikali itaendelea kuwawezesha vijana kwa kuwatengenezea mazingira mazuri ya mikopo ili waweze k...