Jumatatu, 17 Julai 2017

HALMASHAURI YA WILAYA MUFINDI YAPONGEZWA HATI SAFI



Na. Mwandishi Maalum, Iringa
Halmashauri ya wilaya ya Mufindi yapongezwa kwa kupata hati safi ya ukaguzi kwa hesabu za serikali zilizoishia Juni, 2016 na kutakiwa kudumisha ushirikiano ili rasilimali za Halmashauri ziendelee kutumika kwa manufaa ya wananchi.

Pongezi hizo zilitolewa na mkuu wa mkoa wa Iringa, Amina Masenza katika hotuba yake aliyoitoa katika kikao cha baraza la madiwani la Halmashauri ya wilaya ya Mufindi kujadili taarifa ya mdhibiti na mkaguzi mkuu wa hesabu za Serikali kwa hesabu zilizoishia tarehe 30 Juni, 2016 wilayani Mufindi.
 
Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Amina Masenza
Masenza alisema “mheshimiwa mwenyekiti, nichukue fursa hii kwa namna ya pekee kabisa kuipongeza Halmashauri ya wilaya ya Mufindi kwa kupata hati safi ya ukaguzi kwa hesabu za serikali zilizoishia tarehe 30 Juni, 2016. Hongereni sana”. 

Aliitaka Halmashauri hiyo kuendeleza ushirikiano uliopo baina ya madiwani na watendaji wa Halmashauri ili rasilimali za Halmashauri ziwanufaishe wananchi. Aidha, aliitaka Halmashauri hiyo kuendelea kuboresha na kuimarisha mifumo ya udhibiti wa ndani ili iweze kupata hati safi kila mwaka.

Mkuu wa mkoa wa Iringa aliitaka Halmashauri hiyo kuhakikisha hoja zote za miaka ya nyuma zinafanyiwa kazi na kuhakikiwa na na kufungwa na mkaguzi wa hesabu za Serikali. “Kwa mujibu wa taarifa ya mdhibiti na mkaguzi mkuu wa hesabu za Serikali Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi ina hoja 27 za miaka ya nyuma ambazo hazijafungwa na hoja 11 ambazo zimejirudia mwaka 2015/2016” alisema Masenza.

Mkuu wa mkoa aliitaka Halmashauri kuweka utaratibu wa kulipa madeni yanayofikia shilingi 1,269,395,971 yaliyotokana na madai ya wakandarasi, watoa huduma na watumishi kama ilivyobainishwa kwenye taarifa ya mdhibiti na mkaguzi wa hesabu za Serikali. Alishauri mawasiliano yafanyike na Serikali kuu kuona uwezekano wa kulipa sehemu ya deni hilo. Vilevile, aliitaka Halmashauri hiyo kulipa deni la shilingi 193,711,438.40 ambalo ni asilimia 10 ya mapato ya ndani kwenda mfuko wa wanawake na vijana kiasi ambacho hakikupelekwa mwaka 2015/2016. 

Madeni yote ya miaka ya nyuma ya mifuko hii yalipwe ipasavyo kwa kuzingatia agizo la Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC)” alisisitiza Masenza. 

Kikao cha baraza la madiwani la Halmashauri ya wilaya ya Mufindi kujadili taarifa ya mdhibiti na mkaguzi mkuu wa hesabu za Serikali kwa hesabu zilizoishia tarehe 30 Juni, 2016 wilayani Mufindi ni utekelezaji wa agizo la waziri mkuu alilolitoa tarehe 22/4/2017 katika kikao kazi cha baraza la mawaziri cha kujadili taarifa ya ukaguzi ya mdhibiti na mkaguzi mkuu wa hesabu za Serikali ya mwaka 2015/2016.
=30=

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Habari zinazoendelea hivi sasa

SERIKALI KUWEZESHA VIJANA KUKOPA

Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa Serikali itaendelea kuwawezesha vijana kwa kuwatengenezea mazingira mazuri ya mikopo ili waweze k...