Jumatatu, 17 Julai 2017

IRINGA DC KUSAHIHISHA MAPATO YA MIL 400



Na. Mwandishi Maalum, Iringa
Halmashauri ya wilaya ya Iringa imetakiwa kujikita katika kuwasilisha usahihi wa mapato zaidi ya shilingi 400,000,000 yatokanayo na vyanzo vyake jambo lililoisababishia kupata hati isiyoridhisha.

Agizo hilo lilitolewa na mkuu wa mkoa wa Iringa, Amina Masenza katika hotuba yake kwenye kikao cha baraza la madiwani la Halmshauri ya wilaya ya Iringa kujadili taarifa ya mdhibiti na mkaguzi mkuu wa hesabu za Serikali kwa hesabu zilizoishia tarehe 30 Juni, 2016 kilichofanyika katika ukumbi wa Siasa ni Kilimo mjini Iringa.
 
Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Amina Masenza


Masenza alisema “tofauti na hesabu za mwaka 2014/2015, ambapo Halmashauri yenu ilipata hati safi, katika hesabu za 2015/2016 Halmashauri yenu imepata hati isiyoridhisha. Hii ni changamoto kwa Halmashauri ya wilaya ya Iringa. 

Aidha, eneo ambalo lilisababisha msifanye vizuri ni; mkaguzi kushindwa kuthibitisha usahihi wa mapato ya kiasi shilingi 401,554,383 yaliyotokana na vyanzo mbalimbali vya Halmashauri kutokana na kukosekana kwa risiti 38 katika mfumo wa kitabu cha ukusanyaji mapato ya fedha taslimu (MRECOM). Ni imani yangu kuwa, eneo hilo litafanyiwa kazi ipasavyo ili kutoruhusu hali hiyo kujitokeza katika kaguzi zijazo”.

Mkuu wa mkoa wa Iringa aliitaka Halmashauri ya wilaya ya Iringa kufanyia kazi hoja zote za miaka ya nyuma na kufungwa na mkaguzi wa hesabu za serikali wa mkoa. “Kwa mujibu wa taarifa ya mdhibiti na mkaguzi mkuu wa hesabu za Serikali, Halmashauri ya Wilaya ya Iringa ina hoja 39 za miaka ya nyuma ambazo hazijafungwa na hoja 7 ambazo zimejirudia 2015/2016. Hii ni idadi kubwa ya hoja inayohitaji kuweka mpango kazi wa kuzishughulikia na kuhakikisha hoja zote zinafungwa” alisema Masenza.

Aidha, aliitaka Halmashauri ya wilaya ya Iringa kuweka utaratibu wa kulipa madeni yanayofikia kiasi cha shilingi 1,900,180,524 yaliyotokana na madai ya wakandarasi, watoa huduma na watumishi kama yalivyobainishwa na mdhibiti na mkaguzi mkuu wa hesabu za Serikali. Aidha, aliitaka Halmashauri hiyo kulipa deni la kiasi cha shilingi 78,647,303 ambazo ni asilimia 10 ya mapato ya ndani kwenda mfuko wa wanawake na vijana kiasi ambacho hakikupelekwa kwenye mifuko husika kwa mwaka 2015/2016. 

Aliagiza madeni yote ya miaka ya nyuma ya mifuko hii yalipwe kwa kuandaa mpango kazi wa ulipaji wa madeni hayo kama inavyosisitizwa na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC).

Akiongelea udhibiti wa mifumo ya ndani, mkuu wa mkoa aliitaka Halmashauri kuimarisha mifumo ya udhibiti wa ndani ili watumishi wasiostahili kulipwa mishahara na malipo mengine hawalipwi. 

“Taarifa ya mdhibiti na mkaguzi mkuu wa hesabu za Serikali imeonesha kuwa kiasi cha shilingi 2,070,000 kimelipwa kwa watumishi wasiostahili kwa kuwa walikuwa tayari wamestaafu kwa mujibu wa sheria. Aidha, jukumu la Halmashauri katika hili ni kuhakikisha kuwa, wote waliolipwa kimakosa wanarejesha kiasi hicho kilicholipwa kimakosa” aliagiza Masenza. 

Vilevile, aliitaka Halmashauri kupata uthibitisho kutoka Hazina wa kurejeshwa kwa kiasi cha shilingi 16,471,109 ambacho hakikulipwa kwa watumishi kutokana na sababu mbalimbali za kiutumishi.

Kikao cha baraza la madiwani la Halmashauri ya wilaya ya Iringa kujadili taarifa ya mdhibiti na mkaguzi mkuu wa hesabu za Serikali kwa hesabu zilizoishia tarehe 30 Juni, 2016 wilayani Iringa ni muitikio wa agizo la waziri mkuu alilolitoa tarehe 22/4/2017 katika kikao kazi cha baraza la mawaziri cha kujadili taarifa ya ukaguzi ya mdhibiti na mkaguzi mkuu wa hesabu za Serikali ya mwaka 2015/2016.
=30=



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Habari zinazoendelea hivi sasa

SERIKALI KUWEZESHA VIJANA KUKOPA

Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa Serikali itaendelea kuwawezesha vijana kwa kuwatengenezea mazingira mazuri ya mikopo ili waweze k...