Jumapili, 23 Julai 2017

WALIMU WATAKIWA KUCHAPA KAZI WAKATI SERIKALI IKISHUGHULIKIA MADAI YAO



Na. Dennis Gondwe, Iringa
Walimu nchini wametakiwa kuwa wavumilivu na kuendelea kuchapa kazi na kuiamini Serikali inayoongozwa na Rais Dk. John Magufuli kuwa italipa madeni yao kwa mujibu wa taratibu za nchi.

Kauli hiyo ilitolewa na waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako alipokuwa akiongea na walimu na jumuiya ya shule ya sekondari ya wasichana ya Iringa alipofanya ziara ya kikazi mkoani Iringa na kutembelea shule hiyo juzi.

Prof. Ndalichako alisema kuwa Serikali inatambua kuwa walimu wanamadai ambayo hayajalipwa. Alisema kuwa kabla ya kulipa madeni hayo lazima yafanyiwe uhakiki ili kujua uhalali wake. Aidha, aliwataka walimu kufuata taratibu na miongozo ya serikali katika kuwasilisha madai yao na kuhakikisha nyaraka zote halali zinaambatishwa ili kuondoa usumbufu usio wa lazima. 

vilevile, aliwataka walimu kuwa wavumilivu na kuchapa kazi kwa bidii kwa sababu Serikali ya awamu ya tano chini ya Rais, Dk. Magufuli italipa madeni yote halali ya walimu. “Naomba tuunge mkono juhudi za mheshimiwa Rais za kutafuta fedha kwa ajili ya watanzania. Tumpe muda mheshimiwa Rais, mambo yatakuwa sawa. Mungu ametupa viongozi wanaotujali” alisema Prof. Ndalichako.

Akiongelea nidhamu na maadili kwa walimu, Prof. Ndalichako aliwakumbusha walimu kuwa wanajukumu la kuwalea wanafunzi na kusimamia maadili yao wenyewe na wanafunzi. “Walimu ni wazazi na walezi, hivyo mnalo jukumu la kuwalea watoto hawa wa kike ili waweze kufikia malengo yao. Lazima mjivunie kuacha kumbukumbu nzuri kwa wasichana hawa kwa kuwasaidia kufikia mustakabali wa maisha yao” alisema Prof. Ndalichako. 

Wakati huohuo, waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia aliahidi wizara yake kutoa kipaombele kwa mafunzo ya walimu wa lugha za alama ili waweze kujiendeleza kazini.  
=30=

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Habari zinazoendelea hivi sasa

SERIKALI KUWEZESHA VIJANA KUKOPA

Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa Serikali itaendelea kuwawezesha vijana kwa kuwatengenezea mazingira mazuri ya mikopo ili waweze k...