Jumatatu, 17 Julai 2017

ZIMAMOTO YATENGEWA BIL 3 ZA VIFAA



Na. Mwandishi Maalum, Iringa
Serikali imetenga shilingi bilioni tatu kwa ajili ya ununuzi wa mitambo, magari na madawa ya kuzimia moto ili kukabiliana na uhaba wa vifaa kwa Jeshi la Zimamoto na uokoaji nchini.

Kauli hiyo ilitolewa na Kamishna Jenerali wa Jeshi la Zimamoto na uokoaji nchini, Thobias Andengenye alipokuwa akikabidhiwa funguo za gari la Zimamoto na mkuu wa mkoa wa Iringa lililotolewa na Zacharia HansPope katika kituo cha Zimamoto katika Manispaa ya Iringa jana.
 
CGF Thobias Andengenye
Kamishna Andengenye alisema “kwa mwaka wa fedha 2016/2017 Serikali ilitenga kiasi cha shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya ununuzi wa magari mawili ya kuzimia moto na kwa mwaka huu wa fedha jumla ya shilingi bilioni tatu zimetengwa kwa ajili hiyo. Hii ni dalili njema sana na inaonesha jinsi Serikali ilivyo na nia ya dhati ya kuondoa kabisa kama siyo kupunguza kwa kiasi kikubwa upungufu wa vitendea kazi katika Jeshi la Zimamoto na uokoaji”. 

Aliongeza kuwa Serikali inaendelea na mazungumzo na Serikali ya Austria na Ubeligiji ambazo zimeonesha nia ya kutoa mkopo wenye masharti nafuu wa dola za kimarekani 5,000,000 19,000,000 mtawalia kwa ajili ya mitambo na vifaa vya kuzimia moto.

Napenda kutoa shukrani za dhati kwa ndugu Zacharia HansPope, kwa kutoa msaada wa gari aina ya Mercedes Benz lenye ujazo wa lita 5,000 za maji. Huu ni msaada mkubwa sana kwa Jeshi la Zimamoto na uokoaji na mkoa wa Iringa” alisema Kamishna Andengenye. Aliongeza kuwa gari lililokuwa linahudumia katika mkoa wa Iringa lilipata ajali gharama ya matengenezo ni kubwa sana. Aidha, alitoa rai kwa wakazi na wafanyabiashara katika mkoa wa Iringa kushirikiana na Jeshi la Zimamoto na uokoaji hasa wanapoweza kusaidia vifaa ili kuboresha huduma za Zimamoto na uokoaji za kuokoa maisha na mali za wananchi.

Akiogelea matukio ya moto na maokozi, Kamanda wa Zimamoto mkoa wa Iringa, Mrakibu Kennedy Komba alisema kuwa mwaka 2015/2016 matukio ya moto na maokozi yalikuwa 110 ambapo matukio ya moto yalikuwa 90 na matukio ya maokozi ni 20 sawa na 1.1%. Mwaka 2016/2017 matukio ya moto na maokozi yalikuwa 97, ambapo matukio ya moto yalikuwa 83 na matukio ya maokozi yalikuwa 14 sawa na 0.97%. “Kwa ukumla mwaka 2015/2016 na mwaka 2016/2017 kuna upungufu wa matukio kwa 0.13%” alisema Mrakibu Komba.

Mrakibu Komba alisema kuwa upungufu wa matukio ya moto na maokozi unatokana na juhudi za maofisa na askari kufanya ukaguzi wa tahadhari na kinga ya moto kwa njia mbalimbali. Alizitaja njia hizo kuwa ni elimu kwa umma kwa njia ya vyombo vya habari. 

Aliongeza kuwa ofisi yake imeanzisha programu kabambe ya kupitia shule zote za msingi na sekondari katika Manispaa ya Iringa kutoa elimu.
=30=

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Habari zinazoendelea hivi sasa

SERIKALI KUWEZESHA VIJANA KUKOPA

Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa Serikali itaendelea kuwawezesha vijana kwa kuwatengenezea mazingira mazuri ya mikopo ili waweze k...