Jumanne, 15 Agosti 2017

PROF. MAGHEMBE AVUNJA BODI YA MBOMIPA



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Waziri wa maliasili na utalii amevunja bodi ya jumuiya ya hifadhi ya wanyamapori Pawaga na Idodi (Mbomipa)
na kuelekeza katiba ipitiwe upya na kufanyiwa marekebisho yatakayoinufaisha jumuiya hiyo na wananchi kwa ujumla.

Waziri wa maliasili na utalii, Prof. Jumanne Maghembe alitoa kauli hiyo jana katika kijiji cha Tungamalenga alipofanya ziara ya kikazi katika wilaya ya Iringa.

Prof. Maghembe alisema “hakuna bodi ya Mbomipa, kuanzia leo naivunja rasmi bodi ya Mbomipa. Lazima tujipange kujenga bodi mpya ya Mbomipa. Tutengeneze katiba mpya ya Mbomipa ili iendane na sheria ya wanyamapori na kanuni za wanyamapori. Aliongeza kuwa mkinzano wa katiba ya Mbomipa na sheria ya wanyamapori imetoa mwanya kwa bodi kushindwa kutekeleza majukumu yake kikamilifu.

Waziri huyo alitoa siku 20 kwa wataalam wakiongozwa na Mwanasheria wa Halmashauri ya wilaya ya Iringa kupitia upya katiba hiyo na kuiboresha ili iendane na matakwa ya sheria na kanuni za wanyamapori nchini. Alielekeza kuwa baada ya rasimu hiyo kukamilika baraza la ushauri la wilaya, jumuiya ya hifadhi ya wanyamapori Pawaga na Idodi, mkurugenzi wa wanyamapori, mhifadhi mkuu wa Tanapa na afisa wanyamapori wa Halmashauri ya wilaya ya Iringa wakutane na kuipitia rasimu hiyo ya katiba ili ipitishwe.

Prof. Maghembe alisema kuwa baada ya kuvunjwa kwa bodi hiyo, mikataba yote iliyokuwa imeingiwa na bodi iliyopita imevunjwa rasmi. Aidha, aliagiza wawekezaji wote wenye nia ya kuwekeza katika eneo hilo wafuate utaratibu unaokubalika kisheria. Alishauri kuwa bodi inapopitisha mikataba ishauriwe na wanasheria wa mkoa.

Nae mkuu wa mkoa wa Iringa, Amina Masenza aliwataka watakaogombea nafasi katika Mbomipa kujipima kwanza uadilifu wao kabla ya kuamua kugombea. Alisema kuwa tatizo kubwa katika Mbomipa ni udanganyifu. 

Hakuna hata kijiji kimoja kati ya vijiji 21 vinavyounda jumuiya ya hifadhi ya wanyamapori Pawaga na Idodi kilichonufaika na uwepo wa jumuiya hii. Wawekezaji wengi walioingia mikataba na Mbomipa wamekuwa matapeli” alisema Masenza. 

Aliongeza kuwa serikali imeendelea kuhakikisha mbomipa inakuwepo ili kusaidia kudhibiti ujangili katika hifadhi ya Taifa ya Ruaha na maeneo yanayozunguka hifadhi hiyo.
=30=

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Habari zinazoendelea hivi sasa

SERIKALI KUWEZESHA VIJANA KUKOPA

Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa Serikali itaendelea kuwawezesha vijana kwa kuwatengenezea mazingira mazuri ya mikopo ili waweze k...