Jumapili, 28 Januari 2018

MJI MAFINGA WATAKIWA KUFIDIA KUKU WA WANUFAIKA WA TASAF



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Amina Masenza ameiagiza Halmashauri ya Mji wa Mafinga kuwafidia wanufaika wote wa mpango wa kunusuru kaya masikini ambao kuku wao wamekufa kutokana na ugonjwa wa kideri.

Agizo hilo alilitoa katika shule ya msingi ya Mafinga alipofanya ziara ya kuwatembelea wanufaika wa TASAF na kukagua shughuli wanazofanya katika mji wa Mafinga.

Masenza alisema kuwa amepokea kwa masikitiko taarifa zilizotolewa na wanufaika wa mpango wa kunusuru kaya masikini ambao walijinyima na kuanzisha ufugaji wa kuku kwa lengo la kujikwamua, lakini kuku wao wamekufa. 

Naitaka Halmashauri ya mji wa Mafinga kuwafidia kuku wote waliokufa kutokana na kideri na sababu nyingine kwa sababu wataalam wa Halmashauri kushindwa kuwatembelea na kuwashauri vizuri juu ya ufugaji wa kuku” aliagiza Masenza.

Aidha, alitumia kikao hicho kuwaagiza wataalam wa Halmashauri kuwatambua kwa majina, sehemu wanazokaa na shughuli wanazofanya wanufaika wa mpango wa TASAF. 

Watendaji tokeni ofisini na kuwafuata wananchi walipo ili muweze kushauri na kutatua matatizo yao. Lazima mtambue kuwa mpo katika nafasi hizo kwa ajili ya kuwahudumia wananchi. kukaa ofisini wakati wananchi wanashindwa kutatua matatizo yao hamuwatendei haki. Mtaalam yeyote atakayekaidi maelekezo haya anatafuta ugomvi na mimi” alisema Masenza. 

Leticia Sanga ambaye ni mnufaika wa TASAF aliamua kubadilisha mtazamo wa kufuga kuku na kujenga nyumba ya kawaida baada ya kuona kuku alionunua kwa fedha ya TASAF wakifa mfululizo. 

Mimi niliona nijiongeze sababu nilikuwa nafuga kuku lakini kuku wakawa wanakufa hadi kufikia kuku 10. Nikaona nikiulizwa fedha za TASAF nimefanyia nini nitakosa majibu nikaamua kujiongeza kujenga nyumba” alisema Sanga.
=30=

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Habari zinazoendelea hivi sasa

SERIKALI KUWEZESHA VIJANA KUKOPA

Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa Serikali itaendelea kuwawezesha vijana kwa kuwatengenezea mazingira mazuri ya mikopo ili waweze k...