Jumamosi, 29 Aprili 2017

CMT KILOLO KUTOA KIPAUMBELE SUALA LA MAZINGIRA



Na. Dennis Gondwe, KILOLO
Menejimenti ya halmashauri ya wilaya ya Kilolo (CMT) imetakiwa kulipa kipaumbele suala ya uhifadhi na utunzaji wa vyanzo vya maji ili liwe endelevu.

Agizo hilo lilitolewa na mwenyekiti wa kikosi kazi namba tatu cha kunusuru ikolojia ya bonde mto Ruaha mkuu ambaye pia ni Katibu Tawala mkoa wa Iringa, Wamoja Ayubu jana wakati kikosi kazi hicho kilipokutana na timu hiyo katika ofisi ya mkuu wa wilaya ya Kilolo.
Mwenyekiti wa kikosi kazi namba tatu Wamoja Ayubu (kushoto) alifuatilia majadiliano ya wajumbe. Kulia ni Mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya ya Kilolo, Venance Kihwanga


Ayubu alisema “kwenye utoaji wa taarifa za wilaya lazima uzingatie kipaombele cha utambuzi wa vyanzo vya maji na hifadhi ya mazingira kama inavyoelekezwa katika ilani ya uchaguzi ya chama cha mapinduzi”. Alisema ili kufanikisha jambo hilo halmashauri lazima itenge bajeti na kuweka katika mipango suala la ufuatiliaji na usimamizi wa vyanzo vya maji na uhifadhi wake.

Mwenyekiti huyo aliutaka uongozi wa halmashauri hiyo kuendelea kuwaelimisha wananchi juu ya umuhimu wa uhifadhi na utunzaji wa vyanzo vya maji. Alisema kuwa uelimishaji huo lazima uwe shirikishi ukishirikisha viongozi wa chama tawala, wadau na ukijikita kwa viongozi wa kisiasa na kijamii. “Wataalamu wenzangu lazima tusimame kwenye taaluma zetu katika kutekeleza majukumu yetu ili kunusuru uharibifu wa mazingira” alisisitiza Ayubu.

Awali Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Kilolo, Aloyce Kwezi alisema kuwa halmashauri hiyo ina jumla ya vyanzo vya maji 1,630. Alisema kuwa kati ya vyanzo hivyo vya maji, vyanzo 938 ndiyo vinavyopewa msisitizo mkubwa.

Alisema kuwa halmashauri yake inakabiliana na changamoto kubwa mbili na kuzitaja kuwa ni uchomaji moto ovyo misitu na kilimo katika vyanzo vya maji. Alisema kuwa halmashauri yake imejikita katika kutoa elimu kwa wananchi juu ya umuhimu wa utunzaji wa vyanzo vya maji na mazingira kwa ujumla.

Aidha, aliongeza kuwa halmashauri yake inatambua kuwa mpango wa matumizi bora ya ardhi ni njia ya kutatua migogoro ya ardhi na uhifadhi wa maziringa. “Hadi sasa vijiji 38 kati ya vijiji 109 vimefanyiwaa mpango wa matumizi bora ya ardhi” alisema Kwezi.

Kikiwa wilayani Kilolo kikosi kazi hicho kilikutana na kupokea maoni ya kamati ya usalama ya wilaya, timu ya menejimenti ya halmashauri, wanasiasa na wakulima na wafugaji wakubwa wa mashamba ya mifugo wilayani humo.
=30=

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Habari zinazoendelea hivi sasa

SERIKALI KUWEZESHA VIJANA KUKOPA

Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa Serikali itaendelea kuwawezesha vijana kwa kuwatengenezea mazingira mazuri ya mikopo ili waweze k...