Jumatano, 13 Septemba 2017

WANUFAIKA WA TASAF IRINGA MANISPAA WATAKIWA KUJITATHMINI



Na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Wanufaika wa mpango wa kunusuru kaya masikini kupitia TASAF Manispaa ya Iringa wametakiwa kutathmini manufaa waliyopata kupitia fedha wanazopewa na mpango huo.

Kauli hiyo ilitolewa na mkuu wa mkoa wa Iringa, Amina Masenza alipofanya ziara maalum ya kuwatembelea wanufaika wa mpango wa kunusuru kaya masikini katika mtaa wa Ngelewala uliopo Kata ya Mwangata Manispaa ya Iringa leo.

Masenza alisema “kila mnufaika anayepokea pesa za TASAF lazima ajitathmini, fedha hizo zimemsaidia nini? Kama hakuna basi ujue ipo kasoro”. Alisema kuwa serikali inatoa pesa hizo ili ziwasaidie wanufaika kuondoka katika hali duni ya maisha kuelekea hali bora. Alishauri kuwa pesa hizo zitumike kwa uangalifu ili zilete matokeo yaliyokusudiwa.

Mkuu wa mkoa aliwataka watendaji wa mitaa kuwa karibu na wanufaika wa mpango wa kunusuru kaya masikini ili kuwasaidia na kuwashauri vizuri. “Ni jukumu la kila mtendaji wa mtaa kujua hitaji la kila mnufaika wa TASAF. Wapo wanufaika wanaotaka kufuga lakini hawajui wanaanzia wapi, wapo wanufaika wanaohitaji kulima lakini hawajui waanzie wapi, hivyo kuwa nao karibu kutawasaidia kufikia malengo yao” alisema Masenza.

Akiwasilisha taarifa fupi ya mpango wa kunusuru kaya masikini TASAF awamu ya tatu, mratibu wa TASAF Manispaa ya Iringa, Lucy Mtafi alisema kuwa mpango huo umelenga kuziwezesha kaya masikini kupata mahitaji ya msingi na fursa za kuongeza kipato, kulinda rasilimali zao na kuweka akiba kwa ajili ya kujiletea maendeleo na hatimae kujitoa katika umasikini.

Mtafi alisema kuwa mitaa ya Mawelewele na Ngelewala inayotembelewa na mkuu wa mkoa ina wanufaika 77 ambao walipokea ruzuku ya shilingi 28,928,000.

Akiongelea mafanikio yaliyopatikana, mratibu wa TASAF Manispaa ya Iringa, aliyataja kuwa ni kuongezeka kwa mahudhurio ya wanafunzi shuleni kutoka 80% hadi 99%. 

Aliongeza kuwa wazazi wamemudu kununua mahitaji ya watoto ya shule. Mafanikio mengine aliyataja kuwa ni mahudhurio ya kupima watoto kliniki yameongezeka kwa 90% na elimu ya lishe bora imetolewa kwa akina mama wanapohudhuria kliniki. Jumla ya kaya 2,302 zimejiunga na mfuko wa tiba kwa kadi (TIKA) na wanufaika wa wamemudu kupata mahitaji ya msingi kama milo mitatu kwa siku. Mengine ni wanufaika kuanzisha biashara ndogondogo na ufugaji wa kuku na nguruwe.  

Mpango wa kunusuru kaya masikini katika Manispaa ya Iringa ulizinduliwa tarehe 6/1/2015.
=30=
 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Habari zinazoendelea hivi sasa

SERIKALI KUWEZESHA VIJANA KUKOPA

Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa Serikali itaendelea kuwawezesha vijana kwa kuwatengenezea mazingira mazuri ya mikopo ili waweze k...